Muuguzi aliyetumbuliwa kwa vyeti feki mbaroni kwa kumtoa mimba mwanafunzi na kumsababishia kifo

Jeshi la polisi mkoani Kagera linamshikilia Dezber Kahwa mwenye umri wa miaka 49 mkazi wa kijiji Kibengwe, Bukoba Vijijini kwa tuhuma za kusababisha kifo cha Alinda Leverian mwenye umri wa miaka 14.

Aliyeuawa ni mwanafunzi wa darasa la sita Shule ya Msingi Kilima, ambapo mtuhumiwa huyo alimtoa mimba kwa njia isiyokuwa halali na salama.

Kamanda wa Polisi mkoani Kagera, Revocatus Malimi amesema kuwa tukio hilo lilitokea Februari 08 mwaka huu nyumbani kwa Vedastina Cleophace, huku Kahwa ambaye alikuwa muuguzi katika zahanati ya Buza kabla ya kufukuzwa kazi na serikali wakati wa kuwaondoa watumishi hewa, kujaribu kumtoa mimba mwanafunzi huyo.

Mwili wa mwanafunzi huyo umefanyiwa uchunguzi na daktari wa binadamu katika hospitali ya Rufaa Bukoba na kubaini kuwa chanzo cha kifo hicho ni kutobolewa kwa mfuko wa uzazi na kuingizwa sumu.