https://monetag.com/?ref_id=TTIb Mwiko mwalimu kumfanya mpenzi mwanafunzi- RC Malima | Muungwana BLOG

Mwiko mwalimu kumfanya mpenzi mwanafunzi- RC Malima


Na James Timber, Mara.

Mkuu wa Mkoa wa Mara Adam Malima amewataka walimu kuacha mara moja mahusiano ya kimapenzi na wanafunzi kwani kwani jambo hilo linapelekea mwanafunzi kutokufanya vizuri kwenye masomo na kudidimiza kiwango cha ufaulu katika ngazi ya mkoa.

Hayo ameyasema kwenye Kongamano la elimu lililofanyika katika Shule ya Wasichana ya Songe iliyopo Manispaa ya Musoma Mjini, kuwa walimu ni sawa na wazazi hivyo amfundishe mwanafunzi afaulu katika wastani mzuri na siyo kumshawishi kingono.

"Mwalimu ambaye tumekukabidhi mtoto utufundishie tena wa miaka 12 na wewe unaingia naye kwenye mapenzi halafu hapa tunajadili kufeli kwa wanafunzi hamuliweki wakati mnajua kabisa ni changamoto kubwa inayopelekea matokeo mabaya ya mwanafunzi," amesema Malima.

Kwa upande wake Profesa Sospeter Muhongo, ambaye ndiye alitoa wazo la kongamano la kujadili ufaulu wa wanafunzi mkoani akiwaunganisha walimu, wanafunzi, wazazi, wadau wa elimu na viongozi mbalimbali wa kisiasa pamoja na Taasisi binafsi, amewataka wote kuongea lugha moja na kutatua tatizo la elimu ambapo Mkoa wa Mara imeshika nafasi ya mwisho kwa miaka mitatu mfulilizo kwenye mitihani ya kitaifa.

Hata hivyo baadhi ya walimu wamesema kuwa wazazi hawatoi ushirikiano wa kutosha kwa wanafunzi huku wakiwatishia walimu kwamba watawafanyia vitu visivyofaa kupitia imani za kishirikina kama watawapa adhabu watoto wao jambo linalowaogopesha walimu kufundisha darasani.

Aidha moja kati ya wanafunzi aliyetambulika kwa jina la Suzan Robert kutoka shule ya wasichana ya Tarime ameeleza kuwa kufeli kwao kunachangiwa na baadhi ya wazazi kuwakeketa watoto wa kike jambo na kupelekea mwanafunzi kuwa na msongo wa mawazo ikiwemo kutofanya vizuri kitaaluma afikiapo umri wa kukeketwa.