Vifo vya Corona vyafikia 1523 China


Beijing China leo imetangaza kuwa maambukizi ya virusi vya Corona yamefikia visa 66,492 huku idadi ya waliokufa imepanda hadi watu 1,523 na wagonjwa wengine 11,053 wako kwenye hali mahututi.

Hata hivyo takwimu zilizotolewa zimeonesha kupungua kwa idadi ya maambukizi mapya ikilinganishwa na zile zilizotolewa siku moja iliyopita.

Lakini kulingana na takwimu hizo idadi ya vifo bado inapanda na katika kipindi cha masaa 24 yaliyopita vifo vipya 143 vilirikodiwa.Kwa mara ya kwanza siku ya Ijumaa, China ilitangaza takwimu za maambukizi ya virusi vya Corona kwa wafanyakazi wa afya na kuthibitisha zaidi ya watumishi 1,700 wafanyakazi wa hospitali wameambukizwa virusi hivyo.

Virusi vya Coorna vilivyozuka kwenye mji wa Wuhan Disemba iliyopita tayari vimesambaa kwenye mataifa kadhaa ulimwenguni na kusababsiha kitisho kikubwa cha afya duniani.