https://monetag.com/?ref_id=TTIb Watu 78,000 waambukizwa virusi vya Corona ulimwenguni | Muungwana BLOG

Watu 78,000 waambukizwa virusi vya Corona ulimwenguni

Shirika la Afya Duniani, WHO limesema watu wapatao 78,000 ulimwenguni wameambukizwa virusi vya Corona. Kwa mujibu wa shirika hilo, idadi ya watu walioambukizwa virusi vya Corona China bara imefikia 76,288 na watu 2,345 wamekufa kutokana na virusi hivyo.

Wakati huo huo, serikali ya Italia imesema inafikiria kuchukua hatua madhubuti kupambana na virusi vya Corona baada ya raia wake wawili kufariki kutokana na ugonjwa huo.

Kifo cha mwanamke mwenye umri wa miaka 75 kilichoripotiwa jana karibu na mji wa Codogno huko Lombardy kimetokea siku moja baada ya mwanaume mwenye umri wa miaka 78 kufariki kutokana na virusi hivyo kwenye mkoa jirani wa Veneto.

Mripuko wa Corona nchini Italia, umesababisha huduma katika miji kadhaa kusimamishwa, huku kukiwa na ongezeko la wagonjwa 40 walioambukizwa.

Waziri Mkuu wa Italia, Giuseppe Conte ameelezea kusikitishwa na vifo hivyo na ameitisha mkutano wa dharura.