Mwili waokotwa Ziwa Victoria, Padre aelezea tukio


Kamanda wa Jeshi la Zimamoto na Uokoaji mkoani Kagera Inspekta Hamis Dawa, amesema kuwa taarifa za mwili wa mwanaume mmoja kuelea Ziwani zilitolewa na Padre Deritius Rwehumbiza wa Kanisa Katoliki Bunena mkoani humo ambalo liko jirani na Ziwa.

Inspekta Dawa ametoa kauli hiyo wakati akieleza taarifa ya Jeshi hilo, kuopoa mwili wa mwanaume mmoja ambaye bado hajafahamika anayekadiriwa kuwa na umri wa miaka 30 hadi 35, aliyezama ndani ya Ziwa Victoria na kisha mwili wake kuelea.

"Sasa hatujui kama ni mvuvi ama ni muogeleaji na sasa Ziwa letu limejaa sana na tumejaribu kutoa elimu kwa wananchi, kutowaachia watoto wao kwenda Ziwani" amesema Kamanda Dawa.

Imeelezwa kuwa mwili wa mwanaume huyo, umehifadhiwa katika Hospitali ya Rufaa ya Mkoa na kuwataka wakazi wa Mkoa huo, kuacha mara moja tabia ya kuogelea Ziwani kwa sasa sababu Ziwa hilo limejaa sana.