Na Omary Mngindo, Bagamoyo.
WANACHAMA 35 wa Chama Cha Mapinduzi (CCM) Jimbo la Bagamoyo Mkoa wa Pwani, wamejitokeza kuchukua fomu za kuwania ubunge katika jimbo hilo, akiwemo aliyemaliza muda wake Dkt. Shukuru Kawambwa.
Zoezi hilo lililoanza Jumatano ya Julai 14, mpaka kufikia Julai 15 saa saba mchana wanachama hao walikuwa wameshachukua fomu hizo tayari kwa mchakato wa kura za maoni ndani ya chama hicho zinazotaraji kufanyika Julai 20 na 21 mwaka huu katika majimbo mawili.
Akizungumza na Waandishi wa habari ofisini kwake, Katibu wa CCM wilayani hapa Gertrude Sinyinza alisema kuwa kwa wilaya nzima ya Bagamoyo waliojitokeza kuwania nafadi hiyo wamefikia 50, ambapo kwa Jimbo la Chalinze waliochukua wamefika 15.
Sinyinza ambaye ameshika nafasi hiyo Julai 14 akiziba nafasi iliyoachwa na Salumu Mtelela aliyeteuliwa kuwa Katibu Tawala wilaya Tarime, alisema kuwa zoezi hilo linakwenda vizuri, huku akiwapongeza baadhi yao ambao wakiwa kwenye ifisi hiyo walikumbatiana na kupiga picha ya pamoja.
"Wanachama wamehanasika sana na wamejitokeza kwa wingi, kwa siku mbili yaani Julai 14 na 15 saa saba mchana tayari wanachama 50 wameshachukua fomu za kuwania ubunge katika wilaya ya Bagamoyo yenye majimbo ya Chalinze na Bagamoyo," alisema Sinyinza.
Aidha aliongeza kuwa kwakuwa bado siku mbili kabla ya mwisho wa zoezi hilo, anaimani kubwa wana-CCM zaidi wataendelea kujitokeza kuwania nafasi hiyo kwenye majimbo hayo, huku akiwaasa kuwa watulivu katika kipindi hiki cha kuelekea kwenye kura za maonina uchaguzi hapo Oktoba mwaka huu.
"Pia nitumie nafasi hii kuwapongeza wana-CCM wenzangu nchi nzima kwa kitendo chetu cha kumpitisha kwa kishindo Mwenyekiti wetu wa Taif Dkt. John Magufuli, hatua inayothibitisha utendaji wake ndani ya chama na nafasi ya Urais," alimalizia Katibu hiyo.
Baadhi ya wana-CCM waliochukua fomu kwa ujumla Mwarami Mkenge, Said Zikatimu, Waandishi wa habari Albart Kawogo na Aboubakary Mlawa, Ramadhani Maneno, Imani Madega, Shukuru Kawambwa na wanachama mbalimbali wa chama hicho.
