Jeshi nchini Lebanon limesema jana kuwa limezuia boti iliyokuwa imewabeba abiria 37 wengi wao kutoka Syria kuondoka nchini humo kupitia baharini, hii ikiwa juhudi ya hivi punde zaidi ya safari ya kuvuka bahari ya Mediterenia.
Boti hilo lilizuiwa siku ya jumamosi usiku karibu na mpaka ulio karibu na bandari ya Tripoli iliyoko katika eneo la Kaskazini mwa nchi hiyo.
Wale waliokuwa wameabiri boti hiyo ni raia 34 wa Syria, wawili wa Lebanon na mmoja wa Palestina huku kukiwa na watoto saba miongoni mwao.
Taarifa kutoka kwa jeshi hilo imesema kuwa mwanamume mmoja wa Lebanon alikamatwa kwa kupanga operesheni hiyo.
Lebanon inayowahifadhi takriban watu milioni 1.5 waliopoteza makazi kutokana na vita katika taifa jirani la Syria, imekuwa ikijizatiti kujikwamua kutoka kwa mzozo mbaya wa kiuchumi na ukosefu wa uthabiti wa kisiasa hata kabla ya kuzuka kwa janga la virusi vya corona.
