Mkuu mpya wa jeshi la Afghanistan chini ya utawala wa Taliban Qari Fasihuddin ameapa leo kuwasambaratisha wapinzani wa kiafghani watakaoiteteresha nchi hiyo kupitia njia za uasi, madai ya haki kwa makundi ya kikabila na demokrasia.
Matamshi ya kamanda huyo wa ngazi ya juu aliyoyatoa kwenye kongamano moja mjini Kabul yamenukuliwa na vyombo kadhaa vya habari nchini Afghanistan pamoja na mitandao ya habari yenye mafungamano na Taliban.
Fasihuddin anayefahamika pia miongoni mwa wapiganaji wa Taliban kama "mbabe wa kaskazini" amesema wapinzani wanalenga kuvuruga usalama na kuitumbukiza Afghanistan kwenye vita vya wenyewe kwa wenyewe.
Mkuu huyo wa jeshi pia amearifu kwamba Afghanistan iko mbioni kuunda jeshi imara litakalokuwa na uwezo wa kuilinda nchi hiyo baada ya kusambaratika kwa jeshi la serikali iliyoangushwa.
