NAIBU Waziri Ofisi ya Rais Utumishi na Utawala Bora, Deo Ndejembi ameridhishwa na namna walengwa wa Mpango wa Kunusuru Kaya Maskini wa Kijiji cha Nia Njema Wilayani Bagamoyo walivyoboresha maisha yao kupitia ruzuku inayotolewa na Mfuko wa Maendeleo ya Jamii (TASAF).
Ndejembi ameyasema hayo wakati akizungumza na walengwa wa TASAF Wilayani Bagamoyo wakati wa ziara yake ya kikazi iliyolenga kukagua utekelezaji wa mpango huo Wilayani humo.
Amesema mafanikio waliyoyapata walengwa hao kwa kujishughulisha na masuala ya ujasiriamali ikiwemo ushonaji wa nguo, ususi na kilimo yanaendana na lengo la Serikali la kuinua Uchumi wa wananchi wake kupitia TASAF.
"Mafanikio mliyoyapata walengwa wa TASAF hapa Bagamoyo yanafurahisha na yanampa nguvu Rais Samia Suluhu Hassan ya kuendelea kuiwezesha TASAF ili wananchi wengi waendelee kunufaika na kuboresha maisha yao.
Nitoe wito pia kwa walengwa wote wa TASAF kushiriki zoezi la Sensa ya Watu na Makazi itakayofanyika Agosti 23 mwaka huu ili kuiwezesha Serikali kupanga mipango ya maendeleo ikiwemo miradi inayotekelezwa na TASAF.
Nyinyi walengwa wa TASAF mnatakiwa kuwa mstari wa mbele kuhamasisha na kutoa elimu kwa wengine ili wajitokeze kushiriki zoezi hili ili Serikali ipate idadi kamili ya watu na kupanga mipango yake ya maendeleo," Amesema Ndejembi.
