Mwanafunzi wa Zambia Lemekhani Nyirenda, aliyefariki mwaka jana alipokuwa akipigania vikosi vya Urusi nchini Ukraine, anatarajiwa kuzikwa siku ya Jumatano.
Nyirenda alikuwa akitumikia kifungo kinachohusiana na dawa za kulevya nchini Urusi lakini aliachiliwa kwa masharti ya kujisajili na kisha kutumwa mstari wa mbele nchini Ukraine.
Mwanafunzi huyo alikufa mnamo mwezi Septemba.
Mazishi yatafanyika wilayani Rufunsa, mashariki mwa Zambia, wiki sita baada ya mwili wake kuwasili nchini humo.
Mama yake Nyirenda, Florence, alisema kanisani wakati wa kuaga mwili katika mji mkuu wa Lusaka, kwamba anamkumbuka sana mwanae ambaye alikuwa wa mwisho kuzaliwa katika familia ya watoto wanne.
"Nitavikumbuka vituko vya mwanangu ambavyo nilivifurahia sana," alisema.
Msemaji wa familia Ian Banda aliishukuru serikali kwa msaada uliotolewa wakati huu wa majaribu.
