Japan yasema meli iliokamatwa na Houthi sio ya Israel ni yao

 


Serikali ya Japan imelaani vikali kutekwa nyara kwa meli ya mizigo inayoendeshwa na Japan katika Bahari Nyekundu na waasi wa Houthi wanaoungwa mkono na Iran.


Wanamgambo wa Yemen walidai kuwa meli hiyo ilikuwa ya Israeli, lakini msemaji wa serikali ya Japani alithibitisha kuwa meli hiyo ilikuwa ya kubeba gari inayoendeshwa na Nippon Yusen.


Katibu mkuu wa baraza la mawaziri la Japan alisema ilikuwa inashughulika ili meli hiyo iachiliwe.


Waziri Mkuu wa Israel Benjamin Netanyahu aliilaumu Iran, ambayo inaunga mkono wanamgambo wa Houthi, kwa utekaji nyara huo.


Bw Netanyahu alisema si meli hiyo wala wafanyakazi hao si Waisraeli, na akataja kuwa ni "shambulio la Iran kwenye meli ya kimataifa".


Watu 22 wanaaminika kuwa ndani ya meli hiyo ambayo inaaminika kumilikiwa na Waingereza.


"Kwa sasa, wizara na mashirika ikiwa ni pamoja na wizara ya uchukuzi na wizara ya mambo ya nje wanakusanya habari na kushirikiana na nchi husika ili kuachiliwa mapema kwa meli hiyo na wafanyakazi wake," Hirokazu Matsuno, katibu mkuu wa baraza la mawaziri la Japan alisema.


Wale waliokuwemo ndani ya ndege hiyo wanaaminika kuwa ni pamoja na Wabulgaria na Wafilipino, na hakuna raia wa Japani miongoni mwa wafanyakazi.


Msemaji wa jeshi la waasi wa Houthi wa Yemen, Yahya al-Sarea, alidai kuwa meli hiyo ni ya Israel na imepelekwa katika bandari ya Yemen.


Awali, Wahouthi walitishia kulenga meli yoyote ya Israel inayoweza kuifikia ili kujibu hatua ya kijeshi ya Israel ya kulipiza kisasi katika Ukanda wa Gaza kufuatia shambulio la Oktoba 7 lililofanywa na wanamgambo wa Hamas.


Israel inasema watu 1,200 wameuawa na zaidi ya 240 kuchukuliwa mateka wakati wa shambulio la kushtukiza la Hamas kusini mwa nchi hiyo.


Israel imeanzisha operesheni kubwa ya kijeshi - inayohusisha mashambulizi ya anga na mizinga pamoja na wanajeshi wa nchi kavu - kwa lengo la kuwaondoa Hamas.


Wizara ya afya inayosimamiwa na Hamas inasema idadi ya waliofariki Gaza tangu wakati huo imefikia 12,300. Zaidi ya 2,000 zaidi wanahofiwa kuzikwa chini ya vifusi.


Waasi wa Houthi wamerusha makombora kadhaa na ndege zisizo na rubani kuelekea Israel mara tu baada ya Israel kuanzisha operesheni yake ya kulipiza kisasi.


Marekani ilisema wakati huo kwamba makombora yote na ndege zisizo na rubani zilinaswa na meli yake ya kivita katika Bahari Nyekundu.

Post a Comment

0 Comments