Maji ziwa Manyara yavamia makazi ya watu, Sillo awapa pole.



Na John Walter -Babati

Mbunge wa Jimbo la Babati vijijini, Naibu waziri wa Mambo ya ndani ya nchi Mhe. Daniel Sillo, amewatembelea na kutoa pole kwa wakazi wa Magara ambao wameathiriwa na Mafuriko yaliyosababishwa na maji  kujaa Ziwa Manyara kutokana na mvua nyingi zinazoendelea kunyesha maeneo mbalimbali nchini.

Sillo ametoa pole hizo  kwa  alipokuwa akizungumza na Wakazi wa  Kijiji cha Manyara na  ikiwa ni ziara yake maalum kuweza kujionea hali halisi ya Mafuriko na uharibifu uliotokea.


Pamoja na hayo amekabidhi magunia 10 ya mahindi akiwataka kuwa watulivu na kusaidiana wenyewe kwa wenyewe  wakati Serikali inapoendelea na utaratibu mwingine.

Mwenyekiti wa Kijiji cha Manyara Juma Jokoda Jorojik amesema takribani wakazi 600 hawana pa kuishi wala chakula kwa kuwa mashamba yao pia yamefunikwa na maji yakiwa na mazao mbalimbali.


Amesema jumla ya kaya 311 zimeathiriwa, mashamba zaidi ya heka 200 zikiwa na Mpunga, mahindi, alizeti na mazao mengine huku kitongoji  cha Kambi ya fisi kikiathiriwa zaidi.


Naye Mkurugenzi mtendaji wa Halmashauri ya wilaya ya Babati Anna Mbogo amewaagiza wataalamu kuendelea kufanya tathmini ya maafa hayo na kumuagiza mganga mkuu wa Halmashauri kuhakikisha wanatia tahadhari kwa Wananchi kuepuka magonjwa ya mlipuko.

Diwani wa kata ya Magara Mheshimiwa Jocob Elias amesema wananchi wamekubwa na adha hiyo tangu januari 2024 kwa sababu maji hayo yanatoka katika mito inayotoka Babati, Ziwa Burunge na Ziwa Manyara.


Katika ziara hiyo Mhe. Sillo aliambatana na Mwenyekiti wa UVCCM Babati vijijini Solomon Mpaki na Katibu wake George Sanka.


Post a Comment

0 Comments