F AGIZO LA RC MANYARA KUHUSU TAA, LAANZA KUTEKELEZWA BABATI. | Muungwana BLOG

AGIZO LA RC MANYARA KUHUSU TAA, LAANZA KUTEKELEZWA BABATI.



Na John Walter-Manyara

Hatimaye kazi ya ukarabati wa taa za barabarani zilizokuwa haziwaki katika Mji wa Babati imeanza kutekelezwa kufuatia agizo la Mkuu wa Mkoa wa Manyara Region kwa Wakala wa Barabara za Vijijini na Mijini (TARURA).

Kwa muda mrefu baadhi ya wakazi wa Babati walilalamikia tatizo la taa za barabarani kuzimika hali iliyokuwa ikisababisha hofu ya usalama nyakati za usiku.

Kufuatia malalamiko hayo, Mkuu wa Mkoa kupitia kikao cha bodi ya Barabara mkoa kilichofanyika hivi karibuni, aliiagiza TARURA kuhakikisha taa zote zilizokuwa haziwaki zinarejeshwa katika hali ya kufanya kazi haraka iwezekanavyo.

Kupitia jukwaa la mitandao la Manyara Mpya, Mkuu huyo wa Mkoa amethibitisha kuanza kwa utekelezaji wa agizo hilo kwa kuchapisha picha zinazoonesha mafundi wakiendelea na kazi ya matengenezo ya miundombinu ya taa hizo.

Akiandika katika ujumbe wake, amesema:

“Ndugu viongozi mliopo mitaani huko Naimani mnaona kazi inaendelea, taa zilizozima ni nyingi na kazi yote itakamilika, tuwe na subra tu. Nawashukuru kwa uvumilivu.
Naimani kwenye hili kikombe kimeniepuka
🙇🏽‍♀️
Nawapenda sana
❤️

Kauli hiyo imepokelewa kwa hisia chanya na wananchi wengi, wakionesha matumaini kuwa kukamilika kwa kazi hiyo kutaimarisha usalama, kuongeza mwanga katika maeneo ya biashara pamoja na kurahisisha shughuli za kijamii nyakati za usiku.

Utekelezaji huo unaonekana kuwa sehemu ya juhudi za uongozi wa mkoa katika kusimamia na kuboresha miundombinu ya huduma za kijamii ndani ya Manispaa ya Babati.

 

Chapisha Maoni

0 Maoni