F BENKI YA TCB YAJIVUNIA UKUAJI WA KASI/YANG'ARA KATIKA SEKTA YA FEDHA/WANAHISA WASHUGHUDIA | Muungwana BLOG
https://c2p.cleverwebserver.com/dashboard/6a0bec4b-79ba-11ef-ad2b-06f0639468d1

BENKI YA TCB YAJIVUNIA UKUAJI WA KASI/YANG'ARA KATIKA SEKTA YA FEDHA/WANAHISA WASHUGHUDIA

 


Na Mwandishi Wetu

BENKI  ya Biashara ya Tanzania (TCB) imejidhatiti kuendelea kuleta mageuzi katika kutumia teknolojia kuchochea ujumuishi wa kifedha hasa kwa wajasiliamali wadogo na wa kati .

Mkurugenzi Mtendaji wa TCB, Bw. Adam Mihayo, alieleza juhudi za kimkakati za benki hiyo ikiwemo kuboresha miundombinu  ya kidijitali pamoja na  kurahisisha upatikanaji wa huduma za kifedha kwa wajasiliamali wadogo na wa kati .

“Kwenye mwaka huu wa fedha, tunalenga kuendelea kuboresha ufanisi katika kutumia fursa zinazotolewa na teknolojia ya kidijitali, kwa lengo la kuwezesha ukuaji wa sekta hii ambayo ni nguzo kuu ya uchumi wa taifa,” alisema Bw. Mihayo wakati wa Mkutano Mkuu wa 33 wa Wanahisa (AGM) uliofanyika jijini Dar es Salaam jana.

Kwa mujibu wa Takwimu za Taifa, SMEs zinachangia zaidi ya asilimia 95 ya biashara zote nchini Tanzania na takribani asilimia 35 ya Pato la Taifa (GDP).

Biashara nyingi kati ya hizo zimeanza kutumia majukwaa mbalimbali ya kidijitali kufanya biashara, hali inayoonyesha umuhimu wa ujumuishaji wa kidijitali katika kukuza sekta hiyo na uchumi kwa ujumla.

Bw. Mihayo aliongeza kuwa benki hiyo imejipanga kuboresha suluhisho za kidijitali zinazowawezesha wajasiriamali na kusaidia maendeleo endelevu, huku ikifanikiwa kupata faida mwaka uliopita.

Faida ya benki hiyo kabla ya kodi ilipanda kwa asilimia 201 hadi kufikia takribani shilingi bilioni 44.81 mwaka jana, kutoka hasara ya shilingi bilioni 44.42 mwaka uliotangulia.

Amesema Mabadiliko haya yanaonesha uboreshaji wa ufanisi wa kiutendaji wa benki pamoja na ongezeko la faida.

Faida baada ya kodi iliongezeka kwa asilimia 170 hadi shilingi bilioni 32.62 mwaka 2024, kutoka hasara ya shilingi bilioni 46.28 mwaka 2023.

Chanzo kikuu cha mafanikio haya kinaonekana kuwa ni ongezeko kubwa la mapato halisi ya riba, yaliyoongezeka kwa asilimia 19.02 hadi kufikia shilingi bilioni 120.90.

“Hii ilitokana na ongezeko la asilimia 16.93 katika mapato ya riba hadi kufikia shilingi bilioni 178.86. Ingawa gharama za riba pia ziliongezeka kwa asilimia 12.79, ongezeko la mapato lilizidi gharama, hivyo kuchangia kwa mafanikio ya kifedha.” alisema .

Aidha, mapato mengine ya kiuendeshaji yalipanda kwa kiwango kikubwa cha asilimia 378.56 hadi kufikia shilingi bilioni 10.47.

Athari ya pamoja ya ongezeko la mapato ya riba halisi na mapato mengine ya uendeshaji ilisababisha mapato ya uendeshaji kupanda hadi faida ya shilingi bilioni 44.81 mwaka 2024, tofauti kabisa na hasara ya shilingi bilioni 44.42 mwaka 2023.

TCB pia ilionesha ukuaji imara wa mizania yake ya fedha. Jumla ya mali za benki ziliongezeka kwa asilimia 25 hadi kufikia shilingi trilioni 1.74, na amana za wateja zilipanda kwa asilimia 23.03 hadi shilingi trilioni 1.17, ishara ya kuongezeka kwa imani ya wateja na shughuli za biashara.

Wakati uwiano wa mikopo chechefu kwa jumla ya mikopo uliongezeka kidogo hadi asilimia 3.08, bado uko ndani ya  kiwango na Banki Kuu ya Tanzania ambacho ni asilimia 5.0.

Mwenyekiti wa Bodi wa Benki hiyo Martin Kilimba amesema  TCB itaendelea kujizatiti kutoa  suluhisho la mahitaji mbalimbali ya kifedha katika kuchangia mafanikio ya Watanzania.

“Katika mwaka huu wa fedha; tunakusudia kuendelea kuboresha ufanisi wetu …
Malengo yetu ni kuendelea kuboresha mizania, kujenga taswira mpya ya taasisi yetu, kutumia fursa zinazoletwa na teknolojia ya kidijitali,” alisisitiza.

Mwisho.

Post a Comment

0 Comments