Na John Walter-Babati
Benki ya CRDB kupitia CRDB Foundation imezindua rasmi
mpango wa kutoa mikopo isiyo na riba kwa ajili ya uwezeshaji wa wanawake,
vijana na watu wenye mahitaji maalum, uzinduzi uliofanyika leo katika Halmashauri
ya Wilaya ya Babati mkoani Manyara.
Mpango huo unalenga kuwawezesha wananchi kiuchumi kupitia
utoaji wa mitaji sambamba na mafunzo ya elimu ya fedha, ikiwa ni pamoja na
namna ya kutunza fedha, kuweka kumbukumbu za biashara, kuandaa bajeti na uelewa
mpana wa masuala ya fedha ili kuhakikisha mikopo hiyo inaleta tija kwa
walengwa.
Akizungumza katika uzinduzi huo, Meneja wa CRDB Kanda ya
Kaskazini, Cosmas Saadat, amesema mafunzo ya elimu ya fedha yatakuwa endelevu
kwa wanufaika ili kuwajengea uwezo wa kuendesha na kukuza biashara zao kwa
ufanisi.
Amesisitiza kuwa kuchukua mkopo ni hatua ya kwanza,
lakini uaminifu katika urejeshaji ni jambo la msingi ili mpango huo uendelee
kuwafikia wananchi wengi zaidi.
Kupitia mpango huo wa IMBEJU, CRDB Foundation
imeshawezesha jumla ya vikundi 154 vya wanawake, vijana na watu wenye mahitaji
maalum, kwa kutoa mitaji yenye thamani ya shilingi milioni 456.
Kati ya hivyo, leo vikundi 12 vilivyosajiliwa katika
Halmashauri ya Wilaya ya Babati vimepatiwa mikopo isiyo na riba yenye jumla ya shilingi
milioni 321 baada ya kukidhi vigezo vilivyowekwa.
Mgeni rasmi katika hafla hiyo, Naibu Spika wa Bunge la
Jamhuri ya Muungano wa Tanzania na Mbunge wa Jimbo la Babati Vijijini,
Mheshimiwa Daniel Baran Sillo, amesema elimu ya fedha ni nyenzo muhimu kwa
wananchi kufanya maamuzi sahihi ya kiuchumi.
Ameipongeza CRDB kwa kutoa mikopo isiyo na riba sambamba
na elimu, akisisitiza kuwa mikopo hiyo irejeshwe kwa wakati ili wananchi
wengine nao wanufaike.
Mheshimiwa Sillo amesema utoaji wa mikopo kwa wananchi ni
moja ya ahadi za Chama Cha Mapinduzi (CCM) katika kampeni za mwaka 2025, na
amewataka wajasiriamali kutokata tamaa bali kuendelea kusonga mbele kwa kuomba
ushauri, kuweka kumbukumbu sahihi za biashara na kuandaa bajeti.
Kwa upande wake, Mkuu wa Wilaya ya Babati, Emmanuela
Kaganda, amesema wanawake ni nguzo muhimu katika utunzaji wa familia na
maendeleo ya jamii, na ameikaribisha CRDB kuendelea kushirikiana na wilaya hiyo
katika utekelezaji wa miradi ya maendeleo.
Naye Mkurugenzi Mtendaji wa Halmashauri ya Wilaya ya
Babati, Anna Mbogo, amesema matarajio ya halmashauri ni kuona mabadiliko chanya
kwa vikundi vilivyonufaika na mikopo hiyo.
Ameeleza kuwa vikundi 12 vilivyokidhi vigezo vitaanza
kupokea mikopo hiyo mara moja, huku akisisitiza uaminifu na urejeshaji wa
mikopo bila “ujanja ujanja”.
Wananchi na wajasiriamali wanaonufaika na mpango huo
wameishukuru serikali pamoja na Benki ya CRDB kwa hatua hiyo ya kuwapatia
mikopo isiyo na riba, wakieleza kuwa itawasaidia kujikwamua kiuchumi na kuinua
maisha yao.

0 Maoni