Na John Walter-Babati
Kiwanda cha sukari cha Manyara Sugar, kilichopo
kijiji cha Matufa, kata ya Magugu, wilaya ya Babati mkoani
Manyara, kimenunua gari lenye mtambo wa kisasa wa kuzima moto
lenye thamani ya shilingi milioni 65.1, ikiwa ni hatua ya kuimarisha
usalama wa kiwanda, wafanyakazi na jamii inayokizunguka.
Akisoma taarifa ya ununuzi wa gari hilo, Afisa Uhusiano
wa Kiwanda cha Manyara Sugar, John Jeu, amesema kuwa uongozi wa kiwanda
umeamua kununua gari hilo kwa fedha zake kama sehemu ya uwajibikaji wa
kijamii na kulinda mali pamoja na maisha dhidi ya majanga ya moto.
Ameongeza kuwa mafunzo ya matumizi ya mtambo huo
yametolewa na Jeshi la Zimamoto na Uokoaji mkoani Manyara ili kuhakikisha
ufanisi katika uokoaji.
Diwani wa Kata ya Magugu, Stanley Charles, amesema
kiwanda cha Manyara Sugar kina mchango mkubwa kwa taifa kwa kutoa ajira nyingi
za muda mfupi na mrefu, hali inayosaidia kuinua uchumi wa wananchi na maendeleo
ya kata hiyo.
Kiwanda hicho kina uwezo wa kuzalisha tani 70 hadi 80 za
sukari kwa siku.
Akizindua rasmi gari hilo, Naibu Spika wa Bunge la
Tanzania na Mbunge wa Jimbo la Babati Vijijini, Mheshimiwa Daniel Sillo,
amesema Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan ameifungua nchi kwa kuweka
mazingira mazuri ya uwekezaji, jambo linalowezesha viwanda kuwekeza zaidi
katika usalama na maendeleo ya jamii.
Mheshimiwa Sillo amekipongeza kiwanda hicho kwa kuunga mkono
jitihada za serikali kwa kutumia na kuzalisha nishati mbadala, pamoja na
kuwasisitiza wananchi wa kata ya Magugu na maeneo ya jirani kuwekeza katika
uzalishaji wa miwa kwa kuwa ni malighafi muhimu kwa uzalishaji wa sukari.
Ameongeza kuwa kiwanda cha Manyara Sugar kina manufaa
makubwa kwa taifa kwa kulipa kodi, kuchangia uchumi wa nchi, na
kuwezesha familia nyingi kuishi kwa furaha kupitia ajira.
Aidha, amekipongeza kiwanda kwa kununua gari hilo
ambalo, licha ya kutumika ndani ya kiwanda, litawahudumia pia wananchi wa
tarafa ya Mbugwe pindi yanapotokea majanga ya moto.
Kwa upande wake, Kaimu Kamanda wa Jeshi la Zimamoto na
Uokoaji mkoa wa Manyara, Kamishna Gilbert Mvungi, amesema jeshi hilo
limewapatia mafunzo na baadhi ya vifaa wafanyakazi wa kiwanda, akibainisha kuwa
ni fahari kuona wadau kama Manyara Sugar wakishirikiana na serikali kupambana
na majanga ya moto na kupanua wigo wa huduma kwa wananchi.
Hizi hapa ni picha mbalimbali wakati wa uzinduzi wa gari hilo la mtambo wa kuzima moto.
0 Maoni