F Serikali yakabidhi vifaa vya tehama kwa idara za ardhi manyara kuboresha huduma kwa wananchi. | Muungwana BLOG

Serikali yakabidhi vifaa vya tehama kwa idara za ardhi manyara kuboresha huduma kwa wananchi.

 


Na John Walter-Manyara

Kamishna wa Ardhi Msaidizi Mkoa wa Manyara, Wenceslaus Ignace Mtui, amekabidhi vifaa vya TEHAMA kwa watendaji wa idara za ardhi katika halmashauri tano za mkoa huo, ikiwa ni jitihada za kuboresha utoaji wa huduma kwa wananchi.

Akikabidhi vifaa hivyo, Mtui amesema Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan ametoa msaada huo kwa lengo la kusaidia upatikanaji wa huduma za ardhi kwa haraka na kwa ufanisi katika halmashauri zote za Mkoa wa Manyara.

Amesema hatua hiyo inalenga kuhakikisha wananchi wanapata huduma bora na kwa wakati, hususan katika masuala ya umilikishaji na usimamizi wa ardhi.

Aidha, Mtui ametoa rai kwa watendaji wa ardhi waliokabidhiwa vifaa hivyo kuhakikisha wanavitumia kwa malengo yaliyokusudiwa na kuvitunza ipasavyo.

Amewasisitiza kufanya kazi kwa weledi na ufanisi ili kuondoa changamoto zinazowakabili wananchi, hususan migogoro ya ardhi ambayo imekuwa ikiathiri maendeleo katika baadhi ya maeneo.

“Ni muhimu kuhakikisha migogoro ya ardhi inamalizika katika maeneo yenu, wananchi wanapatiwa hati zao kwa wakati, na makusanyo ya kodi ya ardhi yanafanyika ipasavyo ili fedha hizo ziweze kutumika kuendelea kuboresha huduma kwa wananchi wengine,” amesisitiza Mtui.

Kwa mujibu wa taarifa hiyo, kila halmashauri imepatiwa kompyuta mbili, UPS mbili pamoja na printa moja.

Vifaa hivyo vinatarajiwa kuongeza ufanisi katika utunzaji wa kumbukumbu, uchakataji wa nyaraka na utoaji wa hati za ardhi.

Hatua hiyo inaonekana kuwa sehemu ya mkakati mpana wa serikali wa kuimarisha sekta ya ardhi na kuhakikisha wananchi wanapata huduma stahiki kwa wakati na kwa ubora unaotakiwa.

 

Chapisha Maoni

0 Maoni