Na John Walter-Manyara
Mwenyekiti wa Halmashauri ya Wilaya ya Babati na Diwani
wa Kata ya Madunga, John Noya, amesema katika kata hiyo wanafunzi wanapaswa
kuzingatia mambo matatu muhimu ambayo ni kusali, kula na kusoma ili
kuongeza kiwango cha ufaulu katika mitihani ya taifa.
Noya ameyasema hayo wakati wa ziara yake ya kutembelea
Shule za Sekondari Utwari, Madunga Girls na Umagi, ambako alizungumza na
wanafunzi pamoja na walimu na kuwapongeza kwa matokeo mazuri ya kitaaluma.
Ziara hiyo pia ilikuwa ni sehemu ya kuwashukuru wananchi
kwa kumchagua kuwa diwani wa kata hiyo.
Amesema baraza la madiwani la Halmashauri ya Wilaya ya
Babati limeweka utaratibu wa kutambua kata zinazofanya vizuri katika mitihani
ya taifa kwa kuzipongeza hadharani, huku zile zinazofanya vibaya zikikumbushwa
wajibu wao mbele ya jamii ili kuongeza uwajibikaji katika sekta ya elimu.
“Nataka ufaulu uongezeke zaidi. Sitaki kuchekwa wala
kuzomewa. Ndiyo maana kwenye baraza letu la madiwani tumekubaliana kuwa kata
zinazofanya vizuri zinapongezwa mbele ya watu, na zile zinazofanya vibaya
zinaitwa pia ili kujitathmini,” alisema Noya.
Amewapongeza walimu, wanafunzi pamoja na wazazi wa Kata
ya Madunga kwa juhudi zao ambazo zimeiwezesha kata hiyo kufanya vizuri
kitaaluma na kuiheshimisha wilaya na mkoa kwa ujumla.
Amewataka kuendelea kuongeza bidii ili kudumisha
mafanikio hayo.
Aidha, Noya ambaye pia ni Makamu Mwenyekiti wa Jumuiya ya
Tawala za Mitaa Tanzania (ALAT) Mkoa wa Manyara, aliwahimiza wanafunzi kusoma
kwa bidii huku akiwataka walimu kuendelea kutimiza wajibu wao kwa weledi ili
kuinua zaidi kiwango cha elimu.
Katika kuhamasisha matumizi ya teknolojia katika elimu,
aliahidi kusaidia upatikanaji wa kompyuta katika shule hizo ili kuwasaidia
wanafunzi kujifunza masomo ya TEHAMA kwa ufanisi zaidi.
Kwa mujibu wa matokeo ya mitihani ya kidato cha nne mwaka
2025 katika Mkoa wa Manyara, Sanu Seminary ilishika nafasi ya kwanza huku Shule
ya Sekondari ya Wasichana Madunga inayomilikiwa na Jimbo Katoliki la Mbulu
ikishika nafasi ya pili kimkoa.
Kwa upande wake, Mkuu wa Shule ya Sekondari ya Wasichana
Madunga, Sr. Devota Maria Sabs, amempongeza Diwani Noya kwa juhudi zake za
kuhamasisha maendeleo ya elimu katika kata hiyo na kuahidi kuwa shule hiyo
itaendelea kufanya vizuri zaidi katika matokeo ya kitaaluma.
0 Maoni