Ebola Yarejea Sierra Leone, 500 kwenye Karantini

Ugonjwa hatari wa Ebola umeibuka tena nchini Sierra Leone ambapo watu zaidi ya 500 wamekwenda kwenye karantini kaskazini mwa nchi hiyo, baada ya mtu mmoja kuthibitishwa kuambukizwa ugonjwa huo.

Mkuu wa kitengo cha mawasiliano katika kituo cha taifa cha kupambana na Ebola Sierra Leone, (NERC) Sidi Yayah Tunis amesema maambukizi hayo yamefanya kijiji kimoja katika wilaya ya Tonkolili kuwekwa kwenye karantini kwa siku 21.

Hassan Abdul Sesay, mbunge kutoka eneo hilo amesema muathirika aliambukizwa Ebola katika mji mkuu, Freetown, na kwamba alikuwa amesafiri kijijini kwa mnasaba wa sherehe za Idul Fitr.

Watu waliowekwa katika karantini ni pamoja na watumishi 30 wa hospitali iliyomhudumia mgonjwa ambaye baadaye alifariki dunia. Kwa mujibu wa serikali ya Sierra Leone, taarifa za wagonjwa watatu zimeripotiwa ndani ya wiki mbili zilizopita.


Kwa mujibu wa takwimu za mwisho za Shirika la Afya Duniani WHO  tangu mwaka 2013 hadi sasa takribani watu 26 elfu wameambukizwa virusi vya ugonjwa huo  huku wengine elfu 11 wakiwa tayari wamepoteza maisha yao aghalabu wakiwa katika nchi za Sierra Leone, Liberia na Guinea Conakry.