Kila kundi la kipato lina tabia na mienendo yake. Pengine
kunakuwa na ugumu wa kuikwepa mienendo hiyo kwa wahusika, baada ya kuingia humo
au mienendo hiyo ndiyo imewasaidia kufika hapo walipofika. Tunasema, kama alivyo binadamu ambapo kila mmoja ana haiba yake,
makundi ya kipato nayo yana haiba zake, ambazo zinaweza kuwa tofauti na makundi
mengine.
Kwa mfano, ukitazama kundi la mabilionea walio wengi
duniani, utabaini kuwa wana sifa ambazo zinajitokeza sana kwa watu hao. Kuna sifa ambazo wanakuwa
nazo na wala hawazipangi, bali ni kwa sababu ya mazingira au saikolojia ya
fedha, wao wanakuwa na tabia au mienendo hiyo zaidi kuliko watu wa makundi
mengine. Kutokana na mienendo hiyo mara nyingi ndiyo inawafanikisha sana .
Ukikagua sana, utakuja kugundua kuwa mabilionea walio wengi ni wale ambao wanafanya biashara
zinazohusiana na fedha, kama benki ikiwa pamoja na uwekezaji wa hisa, kuna
ambao wanasughulikia mawasiliano kama simu na mitandao ya intaneti na hata
kujishughulisha na ujenzi katika kiwango cha kimataifa au kwenye maeneo
mbalimbali kama sehemu muhimu ya biashara zao.
Unaweza ukajiuliza maswali mengi kidogo na kuanza kushangaa
biashara zingine vipi? haziwezi kumpa mtu utajiri na hatimaye kuwa bilionea?
Siyo hivyo, kuwa kwamba biashara zingine haziwezi kumpa mtu ubilionea, hapana.
Hizi ndizo ambazo zimewapa wengi ubilionea zaidi. Ukitazama kwa makini
utagundua ukweli huu kuwa mabilionea wengi wamezalishwa kutokana na biashara
hizo.
Pia mabilionea walio wengi wanatabia za kuacha mali zao kwa taasisi za kusaidia au hata kwenye
nyumba za ibada au mifuko mbalimbali ya misaada baada ya kufa kwao.Na huacha
fedha kidogo sana
kwa watoto wao. Hapa kwetu, watoto wakishakuwa na baba mwenye fedha, hawataenda
shule wala kujifunza maisha. Wanasubiri baba afe ili warithi. Wakati mwingine
hurithishwa hata kabla baba hajafa. Matokeo yake ni kutapanya mali na kubaki
mikono mitupu.
Hata kuna kipindi Bill Gates alishawahi kusema kwamba, hata
iacha fedha yake kwa watoto wake, bali ataitumia kusaidia kuondoa matatizo
yenye kusumbua sana
dunia. Kabla hajafa ameshaanza kufanya hivyo. Watoto wake nao wanahangaika
kivyao kujua maana ya kutafuta. Ni kwa sababu, kuwa sisi, ikiwemo kutafuta
mafanikio kwa bidii zote, ndicho hasa kilichotuleta duniani. Hujaumbwa uwe
maskini.
Lakini lingine la kushangaza zaidi ni kwamba, mabilionea
wengi hawana hata digrii ya kwanza. Inawezekana walipitia vyuo lakini wakapata
cheti au stashahada au walimaliza tu elimu ya msingi au sekondari. Kwa hiyo
utakuja kugundua kuwa, fedha au utajiri hausiani sana
na kusoma sana
na hii inaonyesha haviko karibu. Mawazo, yaani unachoamini kuhusu fedha na
utajiri, ndilo jambo la awali kabisa.
Mabilionea wengi pia hawakupewa urithi au kupata bahati
nasibu katika maisha yao .
Walio wengi wametafuta fedha kwa juhudi
zao wenyewe kwa kuanzia chini kabisa. Wengine waliweza kusota hadi wakawa kama vituko, lakini wakaja kusimama katika njia ambayo
watu wengine wameshangaa na kubakia kusimulia wasielewe ni kitu gani
kilichofanyika.
Kuna tatizo moja kwa mabilionea waliowengi. Kwa kufuata au
kuhangaika kupata mafanikio zaidi, hujikuta wakisahau kwamba, kuna burudani,
kuna ‘hobi’ na muda wa kusahau masuala ya shughuli. Wao ni watu wa kazi tu na
ubunifu ndivyo vyenye kuwaumiza kichwa na si vinginevyo. Kuna wakati huwa
wanajikuta hata wakipunguza hata masaa ya kulala sababu ya kufanya kazi kwa
bidii zote.
Hebu jaribu basi kujikagua ili uone kama ni kweli nawe
unaweza kuwa na sifa kadhaa kama hizo za
mabilionea. Huenda nawe unatamani kuwa bilionea ila hujajua au kuamua ni kwa
njia gani. Jua sifa zao, labda utawea kupima kiwango cha ukaribu wako kwao.
Siyo lazima uwe na fedha nyingi ili kuwa bilionea, anzia hapo ulipo ukiwa
umepania kuwa, unataka kuwa bilionea, utafanikiwa.