Shirikisho la Mpira wa Miguu duniani FIFA limepanga kujadili
lile sakata la daktari wa Chelsea Eva Carneiro aliyechimbwa mkwara na kutolewa
maneno machafu pamoja kufungiwa na kocha wa timu hiyo Jose Mourinho.
Caneiro alitolewa maneno makali na Mourinho baada ya yeye
(Caneiro) na Jon Fearn kuingia uwanjani kumtibia Eden
Hazard wakti Chelsea ilipolazimishwa sare ya
goli 2-2 na Swansea
ikiwa nyumbani Augost 8 mwaka huu.
Kitendo hicho kilisababisha Eden
kutoka nje ya uwanja na kuwaacha wachezaji wa Chelsea wakibaki tisa uwanjani kufutia kadi
nyekundu aliyooneshwa golikipa wa timu hiyo Thibaut Courtois.
Kamati ya madaktari ya FIFA itajadili sakata hilo kwenye mkutano wao
Septemba 11 mwaka huu. Kamati inatarajia kutoa ushirikiano kwa madaktari wa
timu wanaofanya kazi kuhakikisha wachezaji wanakuwa katika hali nzuri.
Mwenyekiti wa kamati hiyo Michael D’Hooghe amesema: “Huu ni
mfano mwingine wa ugumu wa kazi kwa madaktari wa timu”.
“Nataka kujadili suala hili na wenzangu na kuona kama tunaweza kutoa tamko kusaidia madaktari wa timu”.
Mourinho alikosolewa baada ya mchezo huo kumalizika kutokana
na sentensi aliyoitoa kuhusu madaktari wa timu yake kwenye uwanja wa Stamford Bridge lakini hakurudi nyuma wala
hakuomba radhi.