Hii Ndio Sababu ya Tanesco Kukata Umeme Jana

Shirika la Umeme nchini (Tanesco), limetoa sababu ya kukatika kwa umeme katika baadhi ya maeneo jijini Dar es Salaam kuwa imetokana na uunganishaji wa mitambo katika gridi ya taifa.

Akizungumza na Ripota wetu kwa njia ya simu jana, Msemaji wa Tanesco, Adrian Severin, alisema Shirika hilo lilitoa taarifa kwa umma mapema kuhusu kukatika kwa umeme. Alisema katika eneo la Kinyerezi Wilaya ya Ilala, mkandarasi alikuwa akitengeneza mtambo wa umeme ambao utaunganishwa kwenye gridi ya taifa.
Alisema kukatika kwa umeme hakuhusiani na mkutano wa uzinduzi wa kampeni za mgombea urais kupitia Chama cha Demokrasia na Maendeleo (Chadema), Edward Lowassa ambaye pia anaungwa na vyama vinavyounda Umoja wa Katiba ya Wananchi (Ukawa).

“Shirika letu halina uhusiano na siasa na wala halina nia ya kuhujumu Ukawa,” alisema.

Alisema mkandarasi alipewa muda wa kukamilisha kazi hiyo ifikapo Septemba, mwaka huu kinyume na muda huo, Shirika litaingia hasara.