Shirika la Umeme nchini (Tanesco), limetoa sababu ya
kukatika kwa umeme katika baadhi ya maeneo jijini Dar es Salaam kuwa imetokana
na uunganishaji wa mitambo katika gridi ya taifa.
Akizungumza na Ripota wetu kwa njia ya simu jana, Msemaji wa
Tanesco, Adrian Severin, alisema Shirika hilo
lilitoa taarifa kwa umma mapema kuhusu kukatika kwa umeme. Alisema katika eneo
la Kinyerezi Wilaya ya Ilala, mkandarasi alikuwa akitengeneza mtambo wa umeme
ambao utaunganishwa kwenye gridi ya taifa.
Alisema kukatika kwa umeme hakuhusiani na mkutano wa
uzinduzi wa kampeni za mgombea urais kupitia Chama cha Demokrasia na Maendeleo
(Chadema), Edward Lowassa ambaye pia anaungwa na vyama vinavyounda Umoja wa
Katiba ya Wananchi (Ukawa).
“Shirika letu halina uhusiano na siasa na wala halina nia ya
kuhujumu Ukawa,” alisema.
Alisema mkandarasi alipewa muda wa kukamilisha kazi hiyo
ifikapo Septemba, mwaka huu kinyume na muda huo, Shirika litaingia hasara.