Tarehe 7, April ya mwaka 1994 ni mwaka wenye kumbukumbu ya
simanzi na yenye kutia uchungu katika historia ya mwanadamu hapa duniani, kwani
ni mwaka ambao watu takribani 800,000 waliuawa ndani ya siku mia moja.
Ni katika nchi ya Rwanda ambayo ilishuhudia raia
wake, wanawake, kwa watoto wakiuuawa katika hali isiomithilika kutokana na
uroho wa madaraka waliokuwa nao watawala wake.
Pamoja na kuelezwa kuwepo kwa chuki za kikoo baina ya Wahutu
na Watusi, haki za watu kukandamizwa kama
vyanzo vikuu vya mauaji hayo yalioitwa ya kimbari (Genocide), pia vyombo
vya habari vimewekwa katika kumbukumbu za kihistoria kuwa miongoni mwa
vyanzo vikuu vya mauaji na mateso ya
raia wa Rwanda wasiokuwa na hatia.
Katika mauaji hayo ya kimbari vyombo vya habari ambavyo
vingine wahusika wake walifikishwa mbele ya mahakama maalumu ya Arusha na
kukutwa na hatia, vilitangaza na kuchapisha habari zilizojaa chuki dhidi ya
wanyarawanda wenyewe, mfano wa gazeti la Kangura, Radio RTLM ambavyo viliandika
kuwa watusi ni mende na walitakiwa kuangamizwa.
Na jambo la kusikitisha sana mataifa na wale wanaojiita kuwa
ni watetezi wa haki za binadamu
hawakufanya jitihada zozote ili kuokoa roho hizo zilizoangamizwa, bali walikaa
pembeni wakiangalia ushenzi na unyama ukifanywa na watu waliokuwa na roho za
kishetani.
Katika kauli ya ukakasi, Rais wa wakati huo wa Marekani,
Bill Clinton alisema kuwa hawangeweza kuingilia kati kuvizuia vyombo vya
habari vilivyokuwa vikichochea mauaji kwa hoja kuwa vilikuwa vinatumia
haki zao za uhuru wa habari.
Hiyo ni miaka 21 iliopita, iliowaacha wanyarwanda na makovu
ndani ya mioyo yao ya kuwapoteza ndugu, jamaa,
wazazi na mali zao huku
wengine wakifanywa wakimbizi nje ya nchi yao
walioipigania toka mikononi mwa wakoloni wa Ubelgiji.
Vyombo vyetu
Wakati wenzetu wakiwa tayari na historia hiyo mbaya, yenye
kutia uchungu, hapa kwetu vyombo vyetu vingi vya habari vinaonekana kuisahau
kabisa historia hiyo.
Ukiwa huu ni mwaka wa uchaguzi uliojawa na hamasa ya aina
yake kutoka kwa wananchi, vyombo vyetu vingi vya habari hapa nchini navyo
vimejikuta vikikumbwa na ushabiki wakisiasa walionao wananchi wengi kwa sasa.
Vyombo vyetu vingi vya habari kwa sasa vinaonekana
kuitupilia mbali misingi na maadili yao ya kazi, ikiwemo ya
uwazi, uadilifu na kutokuwa na upendeleo (Objectivity), ushabiki kipindi
vinapoandika habari zao nyingi zikiwemo za kisiasa.
Vimejisahau kuwa navyo ni sehemu ya jamii na vinapaswa
kuitumikia jamii kwa kuhakikiksha vinaandika habari zenye kuilea na kuijenga
jamii katika msingi ilio bora isiokuwa na mitafaruku inayozalishwa na vyombo
hivyo.
Ninasema vimejisahau, kwani tayari tumeanza kuziona habari
zenye viashiria vya chuki kwa jamii, mfano ni ile habari ilioandikwa na moja ya
magazeti ya muda mrefu hapa nchini eti kuwa wananchi waliojitokeza kwenda
kumsindikiza mgombea wa Urais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kupitia chama
cha Demokrasia na Maendeleo(CHADEMA) Ndugu Edward Lowassa kwenda kuchukua
fomu eti walikuwa ni vibaka, kichwa cha
habari kikasomeka, “Vibaka watikisa jiji la Dar Es Salaam”.
Gazeti lingine mara baada ya CCM kutangaza timu ya watu wake
wa kampeni, likaandika habari yenye kichwa cha habari kuwa “CCM Yaunda timu ya ‘kumtusi’ Lowassa.”
Zipo habari nyingi tu zimekuwa zikiandikwa kwa mrengo ambao
ni wa kiushabiki na usio na ukweli wowote, kama kweli wale wafuasi wa Lowassa
ingethibitika ni vibaka kweli, hakuna jinsi ukweli lazima usemwe, na kama kweli
timu ya CCM ni ya kumtusi Lowassa,
hakuna jinsi lazima ukweli usemwe.
Ila sidhani kama kuna chombo hata kimoja kati hivyo, kina
ushahidi wa habari zao hizo, kama sio ushabiki tu usio na maana, kama ni
uchambuzi nadhani nafasi yake ilikuwa ni kwenye makala japo nako huko ukweli
huzingatiwa pia sio uchambuzi tu.
Na kama inavyofahamika, miongoni mwa nadharia
zinazozungumzia jinsi vyombo vya habari vinavyoathiri hadhira zao ni ile iitwayo nadharia ya risasi (Magic
Bullet Theory) ambayo athari(ujumbe) zake huwafika walengwa kama risasi na kwa
kuamini moja kwa moja kile kilichoandikwa pasi na kuifanyia tathmini ya kina
habari hiyo.
Na kama nilivyotanabaisha
hapo juu kuwa huu ni mwaka wa uchaguzi, ambao umejawa na hamasa na ushabiki wa
aina yake, hivyo wananchi wengi wamebaki kuwa ni wakupokea na kuamini kila
kinachosemwa, hawataki kufanya tafakari dhidi ya habari husika, ilimradi iko
upande wake.
Mfano, mara baada ya kuandikwa kwa habari hiyo ya kuwa timu
ya kampeni ya CCM ni ya kumtusi Lowassa, nilikuwa katika sehemu wanapouza
magazeti hapa jjini Dar Es Salaamu, nilichokiona wengi waliiamini habari hiyo
na ubishi mkubwa ukazuka baina ya wafuasi wa vyama huku kauli ikiwa “Wajaribu
kumtusi Lowassa waone.”
Uhariri hatari
Pia nimeshangazwa sana
kumuona mmoja wa wahariri hapa nchini wakati akiongea kwenye runinga moja hapa
nchini , akitetea vyombo vya habari vya kibinafsi kuchukua upande kwa kuandika habari kama
wao wanavyotaka, huku akitilia mkazo tu kwa vyombo vya habari vya umma ndio
vinapaswa kuandika habari zenye usawa bila kupendelea chama chochote.
Nadhani alijasahau kwani kwa mujibu wa misingi na maadili ya
uandishi wa habari, ni wajibu wa kila mwandishi wa habari na chombo cha habari
bila kujali hiki ni cha kibinafsi, na kile ni cha umma kuandika habari yeneye
ukweli, mizani sawa na kutokuwa na upendeleo (impartiality).
Bado kuna muda
Hadi hapa tayari vyombo vya habari vimeshaanza kuigawa jamii
kulingana na habari vinavyoandika, na huu ni mwanzo tu, kampeni ndio zimeanza.
Bila kuwakumbusha wahusika wa habari tutegemee habari nyingi za kuigawa jamii.
Mwisho wake unaweza kuwa ni mbaya, hivyo vyombo vyetu navyo vikumbushwe historia
hii ya Rwanda .
Visije vikatupeleka huko.