Mgombea udiwani wa Kata ya Bomang’ombe wilayani Hai kwa
tiketi ya Chama cha Mapinduzi (CCM), Livingstone Nkya maarufu kama
Ferefere, amefariki dunia ghafla muda mfupi baada ya kuzindua kampeni zake za
kuwania nafasi hiyo.
Ferefere alifariki jana jioni baada ya kukimbizwa katika
Hospitali ya Rufaa ya KCMC ya mjini Moshi, kwa ajili ya kupatiwa matibabu.
Katibu wa CCM Wilaya ya Hai, Allan Kingazi, alilithibitishia
Nipashe kwa njia ya simu jana kuwa, mgombea huyo aliaga dunia baada ya kuzindua
kampeni za uchaguzi kwenye kata hiyo.
Alisema Ferefere alianza kuhisi afya yake inabadilika na
kumfanya kushindwa kuendelea na jukumu la kujieleza, hivyo aliamua kuondoka
baada ya mkutano huo na kwenda kutibiwa katika Hospitali ya Mkoa wa Kilimanjaro
ya Mawenzi, kabla ya kuhamishiwa KCMC.
Kata ya Bomang’ombe ni miongoni mwa kata mpya tatu
zilizogawanywa katika Jimbo la Hai, lililokuwa likiwakilishwa bungeni na
Mwenyekiti wa Taifa wa Chama cha Demokrasia na Maendeleo (Chadema), Freeman
Mbowe.
“Ni kweli mgombea wetu amefariki jana usiku katika Hospitali
ya Rufaa ya KCMC majira ya jioni; na hivi sasa tuko kwenye taratibu za kuandaa
mazishi yake. Tunasubiri majibu ya daktari kujua amefariki dunia kutokana na
tatizo gani, lakini sisi kama CCM
tutasimamisha mgombea mwingine ili kutwaa kata hiyo,”alisema Kingazi
Msimamizi wa uchaguzi wa jimbo la Hai, Said Mderu
alipotafutwa na NIPASHE ili kutoa ufafanuzi iwapo uchaguzi huo utaahirishwa au
laa, alisema,” Mimi sina taarifa za kifo hicho na kwa sasa nipo njiani, siwezi
kuzungumza lolote. Nitafute kesho (leo) nitakuwa na majibu.
Ferefere ambaye pia ni mfanyabiashara maarufu wa maduka ya
vileo na vinywaji baridi mjini hapa, alikuwa akigombea kiti hicho, akishindana
na mgombea wa Chama cha Demokrasia na Maendeleo (Chadema), Joe Nkya ambaye naye
ni mfanyabiashara wa maduka ya pembejeo za kilimo.