Vioja katika mikutano ya kampeni za uchaguzi mkuu vimezidi
kujitokeza ambapo jana mgombea ubunge katika Jimbo la Iramba Magharibi, Mwigulu
Nchemba, amejikuta akimwaga sera kwa kutumia lugha ya Kinyiramba badala ya
Kiswahili kama Sheria za uchaguzi zinavyosema.
Nchemba alitumia lugha ya Kinyiramba kwa madai ya kuwa
anaweka msisitizo kwa wapiga kura ambao walikusanyika katika kijiji cha Kengege
katika jimbo la Iramba Magharibi mkoani Singida.
Akizungumza na wapiga wananchi hao, Nchemba alisema,
atakayeacha kujitokeza kupiga kura wenzake watamsaka ili kujua kwa nini
hakujitokeza siku ya kupiga kura.
Alisema mwaka huu idadi kubwa ya wapiga kura kuwa
wamejitokeza kujiandikisha na kwamba atashangaa kama
siku hiyo watu watalala majumbani mwao badala ya kwenda kupiga kura.
Mwigulu alisisitiza kwamba kila kitu amemalizana na wapiga
kura wake na kwamba wanachosubiri ni kwenda kuichagua CCM siku ikifika.
Hata hivyo, alisema bado kuna tatizo kubwa la maji jimboni
kwake jambo ambalo awamu ya tano ya serikali kama
itakuwa ya CCM italimaliza.
Kwa upande wake, mgombea ubunge katika Jimbo la Singida
Kaskazini, Lazaro Nyarandu, alitumia helikopta (Chopa) yenye namba za usajili,
5H-FCG, ambayo iliwavuta wananchi wengi kila ilipotua kwa kuikimbilia.
Akizungumza katika mkutano wa kampeni uliofanyika katika
kijiji cha Msange jimbo la Singida Kaskazini, Nyarandu alisema katika kipindi
cha miaka mitano iliyopita mambo mbalimbali yalifanyika ikiwamo kuboresha
huduma za maji, afya na shule.
Alitoa mfano katika kipindi chake cha miaka mitano ameweza
kuongeza shule kutoka mbili hadi 28 pamoja na kusambaza huduma ya maji na vituo
vya afya.