MJUMBE wa Halmashauri Kuu ya CCM (NEC) na Mbunge wa Urambo
aliyemaliza muda wake, Samuel Sitta ametaka uandaliwe mdahalo kwenye vyombo vya
habari kati yake na mgombea urais wa Chadema, Edward Lowassa uelezwe ukweli juu
ya ukweli wa sakata la Richmond .
Sitta ambaye alikuwa Spika wa Bunge wakati Lowassa
alipojiuzulu kutokana na sakata hilo , alisema
katika mdahalo huo, ataeleza ukweli juu ya uhusika wa Lowassa katika sakata hilo na atatoa vielelezo
kueleza taifa ufisadi uliokuwa ukifanyika.
Alisema hayo jana kwenye ufunguzi wa kampeni za CCM mkoa wa
Shinyanga katika mkutano uliofanyika mjini hapa ambao wagombea wa udiwani na
ubunge wa majimbo yote ya mkoani hapa walitambulishwa.
Katika mkutano huo, alisema kujiuzulu kwa Lowassa mwaka
2008, kulitokana na Kamati Teule iliyoongozwa na Dk Harrison Mwakyembe,
kugundua kwamba fedha za walipa kodi zilikuwa zikipotea bure.
Alisema yuko tayari kusimulia kwa umma utajiri wa mgombea
huyo wa Chadema.
Makundi, urafiki
Sitta ambaye ni Waziri wa Afrika Mashariki, ambaye pia
alikuwa kwenye kinyang’anyiro cha kutaka kuteuliwa kugombea urais kupitia CCM,
alisema wanamwamini Dk John Magufuli katika utendaji wake wa kazi na pia ni
kiongozi asiye na makundi au urafiki.
“Kweli lazima uwapime viongozi, kwani anayetaka urais lazima
achaguliwe kwa kufuata utaratibu, achambuliwe usiogope moshi kama
unapikia kuni…lakini mwenzetu Lowassa hakukubaliana na hayo, akaona kaonewa kwa
madai anafaa kuwa rais mbona sisi tulikubali?,” alihoji Sitta.
Aliendelea kusema, “hali hiyo, ilionesha ndani ya CCM
kulikuwa na vyama viwili ambavyo ni ‘CCM Katiba’ na ‘CCM Maslahi’ ambayo
alikuwa anaongoza Lowassa na mfuasi wake, Mgeja (aliyekuwa Mwenyekiti wa CCM
Mkoa wa Shinyanga ambaye pia alihamia Chadema hivi karibuni).”
Wanachama mapandikizi
Sitta alisema CCM ilikuwa imejaa wanachama walio mapandikizi
tofauti na sasa ambapo alidai wamekwisha jionesha na kimekuwa chama kizuri kama ilivyokuwa enzi za hayati Baba wa Taifa, Mwalimu
Julius Nyerere.
Alisisitiza kwamba kitazidi kuimarika na waliobaki
wataendelea kutetea ilani na kuhakikisha chama kinaendelea kushika dola.
Kwa mujibu wa Sitta, wakati wa mchakato, baada ya kumaliza
vikao, Lowassa alikuwa akiitisha vikao vya kundi lake alilolibatiza CCM Maslahi
na kuwaagiza wapambe wake kuitisha vyombo vya habari kushambulia watu ambao
hawako kwenye mlengo wao.
Wakati huo huo mjumbe huyo wa NEC, alikumbusha umati uliohudhuria
mkutano huo kwamba, uchaguzi wa mwaka huu unatumia Katiba ya zamani ya mwaka
1977 ambayo inatamka matokeo ya rais hayahojiwi hata kama
aliyeshinda, amezidi kura moja.
Sitta ambaye alikuwa Mwenyekiti wa Bunge Maalumu, alisema
alishauri wabunge wasitoke nje ya Bunge hilo
waweze kutumia katiba hiyo iliyokuwa na kipengele cha kuhoji matokeo ya rais
sasa imekula kwao.