Hatimaye Waziri Mkuu Mstaafu, Frederick Sumaye, amesema
kwamba mgombea urais wa Umoja wa Katiba ya Wananchi (Ukawa) kupitia Chama cha
Demokrasia na Maendeleo (Chadema), Edward Lowassa, lazima atashinda katika
uchaguzi mkuu wa Oktoba 25.
Sumaye alitoa kauli hiyo jana asubuhi wakati wa kumnadi
Lowassa kwa wananchi wa Mufindi, mkoani Iringa.
Sumaye, ambaye alishika nafasi ya uwaziri mkuu kwa miaka
kumi katika awamu ya tatu iliyoongozwa na Benjamin Mkapa tangu mwaka 1995 hadi
2005, alisema wananchi wanaojitokeza kwa
wingi katika mikutano ya Lowassa ni kwa sababu wanataka mabadiliko, kwani
hawataka maisha yao yaendelee kuwa kama ya kisiki ambacho huwa hakibadiliki.
“Watanzania wanataka
mabadiliko na mheshimiwa Lowassa lazima atakuwa rais, sisi hatusemi atakuwa
rais kwa kura za bao la mkono bali kwa kura za wananchi ndani ya boksi la
kura,” alisema Sumaye ambaye alijiunga na Ukawa Agosti 21, mwaka huu.
Sumaye alisema Ukawa hawana mpango wa kufanya njama za ovyo
za kuiba kura na kuwaomba wananchi wampe
kura nyingi mgombea wa Ukawa kwa sababu wanahitaji mabadiliko.
Sumaye alisema kwa kuwa Bunge lina wabunge zaidi ya 360,
hivyo ili Lowassa aweze kuunda Baraza lake la Mawaziri, anatakiwa kupata
wabunge zaidi ya 300 na 60 wakitoka vyama vingine na pamoja na idadi kubwa ya
madiwani.
LOWASSA AANIKA VIPAUMBELE
Kwa upande wake, Lowassa alianisha vipaumbele vyake ikiwa
wananchi watampa ridhaa ya kuingia Ikulu.
Lowasa aliwaambia wakazi wa
Mufindi kama wananchi wa Mufindi kuwa
ikiwa watamchagua kuwa rais, atazigeuza kambi zote za Jeshi la Kujenga Taifa
(JKT) kuwa Vyuo vya Ufindi Stadi (Veta).
“Nauliza kwa nini
vituo vyote vya JKT visigeuzwe kuwa vyuo vya Veta na kusoma hapo hapo mambo ya
uzalendo kuna ubaya gani?”alihoji Lowassa huku akishangiliwa na wananchi.
Alisisitiza kuwa kipaumbele cha kwanza hadi cha tatu ni
elimu na kubeza wanaotaka kilimo kuwa kipaumbele cha kwanza.
Lowassa alisema ukombozi
wa kweli wa Mtanzania ni elimu na zawadi nzuri ya mzazi ya kumpa mtoto
wake ni elimu kwani hata katika nchi zilizoendelea kama Singapore, Indonesia na
Malaysia zimesonga mbele kwa sababu ya elimu.
“Watu wajinga hupenda
kuona wenzao wajinga, wanasema kipaumbele ni kilimo kwanza, sasa utampaje mtu
kipaumbele ch kilimo wakati hana elimu?” aliendelea kuhoji.
Alisema serikali yake
itagharimia elimu ya msingi hadi chuo kikuu na mtu asiulize fedha zitatoka wapi
kwani yapo mabilioni ya fedha yanatumika kwa mambo yasiyofaa.
Aliongeza kuwa iwapo watu watakuwa na elimu ya kutosha
itakuwa rahisi kupata ajira.
KUFUTA USHURU WA MAZAO
Kuhusu mazao, alisema akichaguliwa atafuta ushuru wa mazao
na kwamba ni jambo la kushangaza mkulima analima mazao yake halafu serikali
inamkopa.
Akizungumzia kuhusu uchaguzi mkuu wa mwaka huu, alisema wapo
watu wanaosema CCM ni hodari wa kuiba kura na kuwaondoa hofu hiyo kwa
kuwahimiza wananchi watakaokwenda kupiga kura wahakikishe wanazilinda zisiibwe.
“Wapo watu wanasema
CCM ni hodari wa kuiba kura na kwamba wataiba hizo kura halafu nitaanguka,
nataka kila mtu ahifadhi kichinjio chake na siku ya kwenda kupiga kura kila mtu
afanye hivyo, watu wabakie kwenye vituo hadi kura zihesabiwe, tumewasha moto
wanatetemeka,” alisema Lowassa.
Alisema nchi ikikiachia chama kimoja kikatawale kwa muda
mrefu kinawanyanyasa wananchi wake, hivyo wananchi hawanabudi kufanya
mabadiliko kama walivyofanywa raia wa Malawi ,
Zambia na Kenya
waliovipumzisha vyama tawala vilivyodumu madarakani kwa miaka mingi na kuhoji
kwa nini Watanzania wasiweze.
“Vyama vikongwe
vikikaa kwa muda mrefu, wananchi wanateseka, angalia wenzetu wa Malawi, Zambia
na Kenya wamevitoa madarakani vyama tawala, tukikosea tutajutia,” alisema
Lowassa.
MUNGAI AIBUKIA UKAWA, AMPIGIA DEBE LOWASSA
Wakati huo huo;
Mwanasiasa mkongwe nchini na waziri wa zamani, Joseph Mungai, jana
aliibukia katika mkutano wa kampeni wa Lowassa na kumnadi.
Mungai ambaye alitumikia serikali ya awamu ya kwanza, ya
pili na ya tatu, aliibukia katika mkutano huo uliofanyika kwenye Uwanja wa
Shule ya Msingi Wambi na kuanza kumnadi Lowassa.
Mbali na kumnadi Lowassa, Mungai ambaye amekuwa mbunge wa
jimbo la Mufindi kwa miaka mingi, pia alitumia mkutano huo kumnadi mtoto wake,
Willy Mungai, ambaye anagombea ubunge kupitia Chadema katika Jimbo la Mafinga
Mjini.
Willy Mungai anapambana na mgombea wa CCM, Cosato Chumi,
katika jimbo hilo .
Mungai alisema Lowassa na Sumaye ni viongozi ambao wanapenda
sana kusonga
mbele kimaendeleo na hawapendi kubakia hapo walipo na ndiyo maana wameamua
kuhamia upinzani.
“Hawa mawaziri wakuu
mimi nikiwa waziri wao waliniongoza vizuri, ndiyo maana kuna mambo mengi ya
msingi yaliyofanyika katika jimbo hili ikiwa ni pamoja na miradi ya elimu,”
alisema.
Akimnadi mtoto wake, alimtaka kuhakikisha anavaa viatu vyake
ili kuhakikisha wakazi wa jimbo hilo
wanakuwa na maendeleo.
“Nawaombeni wananchi
mumpe mwanangu kura kwa sababu yeye ndiye mwenye uwezo wa kuvaa viatu
nilivyoviacha mimi na siyo mtu mwingine,” alisema.
Mungai alisema ikiwa Willy atashinda, ahakikishe anajenga
uwanja wa mpira wa kisasa ili wananchi wawe wanapata fursa ya kuburudika baada
ya saa za kazi.
Hata hivyo, Nipashe lilipomuuliza Mungai kama
amehamia rasmi Chadema, alisema:
“Mimi ni mwanasiasa
mstaafu, si CCM wala chama chochote cha upinzani.”