Warundi Wapatwa na Hofu ya Kuibuka Vita Nchini

Raia wa Burundi wamepatwa na hali ya wasiwasi mkubwa juu ya uwezekano wa kuibuka vita vya ndani vitakavyoambatana na mauaji makubwa nchini humo.

Kwa mujibu wa televisheni ya Ufaransa, mauaji ya Jenereali Adolphe Nshimirimana aliyekuwa mtu wa karibu wa Rais Pierre Nkurunziza, yamezidisha wasiwasi mkubwa kwa raia wa nchi hiyo masikini ya Afrika ya kati juu ya kutokea vita vya ndani nchini humo. 

Raia wa Burundi wana wasiwasi kwamba, wafuasi wa Nshimirimana watachukua hatua ya ulipizaji kisasi dhidi ya wapinzani wa kisiasa wa serikali na hivyo kuibuka kwa vita. Kufuatia hali hiyo, anga ya usalama nchini Burundi imekuwa tete, wakati huu ambapo fikra za wananchi zinafuatilia nini kitatokea baada ya tukio hilo.


Jenereali Adolphe Nshimirimana aliuawa pamoja na dereva wake asubuhi ya jana baada ya maroketi mawili kulenga gari lake kabla ya kumiminiwa risasi katika eneo la Kamenge mjini Bujumbura. Adolphe Nshimirimana aliwahi kuwa mkuu wa majeshi na alikuwa akifanya kazi katika ikulu ya Rais Nkurunziza. Wapinzani wa serikali wanamtaja Nshimirimana kuwa aliyekuwa na mchango mkubwa katika kumsafishia njia Rais Pierre Nkurunziza kusalia madarakani na kwamba, kama si yeye basi rais huyo asingeweza kugombea muhula wa tatu wa urais.
Mpya zaidi Nzee zaidi

Popular Items

Kilimo cha Bamia