Watanzania wametakiwa kutafakari kwa kina kauli iliyotolewa
na mgombea wa kiti cha urais kupitia UKAWA Mh Edward Lowassa ya kuwaachia huru
baadhi ya watuhumiwa wa makosa ya kigaidi yaliyosababisha vifo na ulemavu wa
kudumu kwa baadhi ya viongozi wa dini wa kiislamu na kikristo pamoja na wageni
kutoka nje ya nchi sambamba na watuhumiwa wengine wa makosa ya kijinai bila
kujali athari zinazosababishwa na matukio ya kigaidi ulimwenguni.
Tahadhari hiyo imetolewa mjini Ludewa mkoani Njombe Bwana
Amoni Mpanju wakati akizungumza na mamia ya wananchi waliojitokeza kusikiliza
sera za Dr Magufuli na kuongeza kuwa wakati dunia ikihaha kupambana na janga la
matukio ya kigaidi yanayosababisha vifo na ulemavu wa kudumu kwa binadamu bila
ya kujali imani zao za kidini na mataifa yao baadhi ya viongozi wanaowania
kuliongoza taifa la Tanzania wanatangaza hadharani kuwaachia huru watuhumiwa wa
ugaidi waliosababisha vifo na majeruhi kwa viongozi wa dini za kikristo na
kiislamu na wageni wa mataifa mengine na kuwataka watanzania kutafakari kauli
hiyo ya Mh Lowassa.
Dr John Pombe Magufuli akiwa katika ubora wake amefanya
mikutano zaidi ya mitano akiwa njiani kutoka mkoano Njombe kuelekea Ludewa
Songea kwa njia ya barabara ambapo amekuwa pia akisikiliza kero za walemavu
alioonana nao na kuongeza kuwa uongozi ni msalaba na si kila mtu anaweza
kuwatumikia kwa dhati wananchi na kwamba kiongozi anapaswa kuzifahamu kero za
wananchi na kuziishi na kwamba ili Tanzania iwe na amani ni lazima majeshi yetu
yaendeshwe kisayansi na kuahidi kuayaboresha.
Aidha Dr Magufuli ambaye amekuwa akishangiliwa na umati
mkubwa wa wananchi waliokuwa wanaziba barabara kwa lengo la kutaka kumsikia
amewataka wananchi kumchagua yeye kupitia CCM kwa kuwa ndio chama chenye ilani
bora na ahadi za ukweli huku akiwazodoa UKAWA kwa kutokuwa na ilani ambayo ni
mkataba kati ya watawala na watawaliwa.
Dr Magufuli anatarajiwa kuendelea na ziara yake ya kusaka
ridhaa ya watanzania kuliongoza taifa la Tanzania
ambapo jumatatu ya Septemba mosi anatarajiwa kuendelea na kampeni zake mkoani Ruvuma