Watanzania Watakiwa Kutafakari Kauli ya Mgombea wa UKAWA Kuachia Watuhumiwa

Watanzania wametakiwa kutafakari kwa kina kauli iliyotolewa na mgombea wa kiti cha urais kupitia UKAWA Mh Edward Lowassa ya kuwaachia huru baadhi ya watuhumiwa wa makosa ya kigaidi yaliyosababisha vifo na ulemavu wa kudumu kwa baadhi ya viongozi wa dini wa kiislamu na kikristo pamoja na wageni kutoka nje ya nchi sambamba na watuhumiwa wengine wa makosa ya kijinai bila kujali athari zinazosababishwa na matukio ya kigaidi ulimwenguni.

Tahadhari hiyo imetolewa mjini Ludewa mkoani Njombe Bwana Amoni Mpanju wakati akizungumza na mamia ya wananchi waliojitokeza kusikiliza sera za Dr Magufuli na kuongeza kuwa wakati dunia ikihaha kupambana na janga la matukio ya kigaidi yanayosababisha vifo na ulemavu wa kudumu kwa binadamu bila ya kujali imani zao za kidini na mataifa yao baadhi ya viongozi wanaowania kuliongoza taifa la Tanzania wanatangaza hadharani kuwaachia huru watuhumiwa wa ugaidi waliosababisha vifo na majeruhi kwa viongozi wa dini za kikristo na kiislamu na wageni wa mataifa mengine na kuwataka watanzania kutafakari kauli hiyo ya Mh Lowassa.

Dr John Pombe Magufuli akiwa katika ubora wake amefanya mikutano zaidi ya mitano akiwa njiani kutoka mkoano Njombe kuelekea Ludewa Songea kwa njia ya barabara ambapo amekuwa pia akisikiliza kero za walemavu alioonana nao na kuongeza kuwa uongozi ni msalaba na si kila mtu anaweza kuwatumikia kwa dhati wananchi na kwamba kiongozi anapaswa kuzifahamu kero za wananchi na kuziishi na kwamba ili Tanzania iwe na amani ni lazima majeshi yetu yaendeshwe kisayansi na kuahidi kuayaboresha.

Aidha Dr Magufuli ambaye amekuwa akishangiliwa na umati mkubwa wa wananchi waliokuwa wanaziba barabara kwa lengo la kutaka kumsikia amewataka wananchi kumchagua yeye kupitia CCM kwa kuwa ndio chama chenye ilani bora na ahadi za ukweli huku akiwazodoa UKAWA kwa kutokuwa na ilani ambayo ni mkataba kati ya watawala na watawaliwa.


Dr Magufuli anatarajiwa kuendelea na ziara yake ya kusaka ridhaa ya watanzania kuliongoza taifa la Tanzania ambapo jumatatu ya Septemba mosi anatarajiwa kuendelea na kampeni zake mkoani Ruvuma