Zitto Amshangaa Dk. Magufuli

Kiongozi wa Chama cha ACT-Wazalendo Zitto Kabwe amesema anamshangaa mgombea urais kupitia Chama Cha Mapinduzi (CCM), Dk.John Magufuli kuzungumzia masuala ya barabara kila kukicha  huku masuala muhimu akiyaacha katika kampeni zake.

Amesema mgombea huyo amekuwa akizungumzia zaidi mafanikio na mikakati ya sekta ya ujenzi nchini hususan barabara na kuacha kuizungumzia nafasi ya urais ambayo ni taasisi kubwa.

Akizungumza na waandishi wa habari jana jijini Dar es Salaam, Kabwe alisema, nchi ya Tanzania ina changamoto nyingi ambazo zinahitaji kutatuliwa hivyo mikakati ya chama kinachotarajia kuingia madarakani katika awamu ya tano ni vyema ikawekwa wazi ili umma ufahamu.

Alisema Magufuli hajaweza kutamka wazi jinsi atakavyoweza kutatua kero za wananchi katika sekta ya afya, elimu, uchumi na ajira ambazo ni kikwazo kwa Tanzania kupiga hatua ya maendeleo.

Aidha, alisema jambo moja angalau lililomfanya avutiwe na Magufuli ni kuanzishwa kwa mahakama maalum ya kushughulikia mafisadi.
Hata hivyo, alisema hadhani kama ataweza kulishughulikia suala la ufisadi kwani itamlazimu kuongeza ujenzi wa magaereza kwa kuwa mafisadi ni wengi.

“Sisi ACT-Wazalendo katika uzinduzi wa kampeni keshokutwa (jumapili), tumeweka wazi vuipaumbele vyetu ambavyo ni elimu, afya, kutengeneza mazingira ya uchumi unaozalisha ajira na haki ya kila Mtanzania kuwa na Bima ya afya na kuwa na hifadhi katika mifuko ya hifadhi ya kijamii,’ alisema.

Alisema chama hicho ndiyo chama pekee ambacho kimeandaa ajenda hizo katika kampeni za uchaguzi wa mwaka huu, tofauti na CCM ambayo tayari imekwishaanza kampeni lakini hakuna ajenda zilizopewa vipaumbele.

Katika hatua nyingine, chama hicho kimekata rufaa kufuatia mgombea wake wa nafasi ya ubunge katika jimbo la Kinondoni, Kala pina kuambiwa kuwa hakufikisha vigezo na masharti yaliyowekwa na Tume ya Taifa ya Uchaguzi(NEC).

Alisema kuwa madai ya kuwa mgombea huyo hakupata wadhamini si ya kweli na chama kimeamua kukata rufaa na wanatarajia NEC itaamua kutenda haki katika suala hilo.

“Mgombea wetu wanasema hakupata wadhamini hii si kweli mgombea alipata wadhamini na ushahidi tunao, ni lazima tuwatetee wagombea wetu ambao wameonyesha nia ya kugombea nafasi mbalimbali lakini wakakatishwa tamaa na sababu zisizo za kweli,” alisema.

Chama hicho pia jana kiliendelea kutoa semina ya siku mbili kwa wagombea nafasi za ubunge ambao watawania nafasi hiyo katika majimbo tofauti nchini.

Zitto alisema awamu ya kwanza ya mafunzo hayo yametolewa kwa wabunge 95 huku awamu ya pili ya mafunzo ikiendelea leo kwa wabunge waliobaki.


Chama hicho kinatarajia kuzindua kampeni za uchaguzi Wilaya ya Temeke, Mbagala Zakheem jijini Dar es Salaam na baadaye mikoa ya Pwani, Morogoro, Iringa, Mbeya, Rukwa na Kigoma.