Chama cha ACT Wazalendo kimesema kitashawishi uanzishaji wa
Benki ya Kijamii ya Watu wa Kigoma (Kigoma Community Bank) ili kuwawezesha
wafanyabiashara, wakulima na vikundi vya ujasiriamali kupata mikopo kwa urahisi
na riba nafuu.
Kiongozi Mkuu wa Chama cha ACT Wazalendo, Zitto Kabwe
alisema hayo alipokuwa katika mikutano ya kampeni katika majimbo ya Kigoma
mjini na Buhigwe kuwanadi wagombea wa chama hicho ambao walisema kukamilika kwa
mpango huo kutainua uchumi na maisha ya watu wengi wa Kigoma na mikoa ya
jirani.
“Suala la kuanzisha Benki ya Kijamii kwa Watu wa Kigoma sio
jambo la utani, ni mojawapo ya mikakati kumi ya chama chetu cha ACT Wazalendo
tunayotaka kuitekeleza endapo tutapata ridhaa ya kushinda urais pamoja na viti
vingi vya ubunge,” alisema Zitto.
“Ukienda Mkoa wa Kiliamanjaro utakuta Benki yao ,
Wilaya ya Mwanga katika Mkoa wa Kilimanjaro, Mbinga mkoani Ruvuma
na Mufindi iliyopo Iringa kote huko kuna Benki za Kijamii za maeneo hayo,
tunataka na sisi Kigoma tuanzishe Benki yetu ili isaidie katika kukuza mitaji
ya biashara za watu ambao wamekuwa wakishindwa kupata mikopo katika benki na
taasisi nyingine za kifedha,” aliongeza.
Mkoa wa Kigoma ni miongoni mwa mikoa masikini nchini ikiwa
ni pamoja na mikoa ya Tabora, Singida na Lindi ambayo licha ya watu wake wengi
kuwa na kipato cha chini, imejikuta ikizalisha mazao mengi na kuliingizia taifa
fedha za kigeni kama vile tumbaku na kahawa ambayo yamekuwa muhimili mkubwa wa
uchumi wa nchi.
Alisema Mkoa wa Kigoma ambao una wakulima, wavuvi,
wafanyabiashara na wafugaji unahitaji mtaji wa shilingi bilioni moja ili
kuanzisha benki hiyo.