Umoja wa Ulaya (EU) umetuma kikosi cha watu takriban 140
watakaofanya uangalizi wa mwenendo wa Uchaguzi Mkuu unaotarajiwa kufanyika siku
23 zijazo.
Waangalizi hao
wanaojumuisha wataalamu mbalimbali wa masuala ya uchaguzi, wanasiasa, baadhi ya
maofisa kutoka balozi za nchi za EU nchini, na waangalizi waliajiriwa kutoka Tanzania ,
watakuwemo nchini hadi mchakato wa uchaguzi utakapokamilika.
Mkuu wa kikosi cha
uangalizi cha EU, (EU EOM), Judith Sargentin amewaambia wanahabari leo kuwa
kikosi hicho kitakuwa na kazi kuu ya kuangalia iwapo uchaguzi utafanyika kwa
kufuata misingi, sheria na kanuni za nchi, za kikanda na zile za kimataifa kama misingi ya kujenga demokrasia.
Amesema tayari baadhi
ya waangalizi walishaanza kuwasili nchini mwanzoni mwa Septemba ikiwemo timu ya
wataalamu wa masuala ya siasa, uchaguzi na sheria zinazohusiana na mchakato wa
uchaguzi iliyowasili nchini Septemba 11.
“Katika kipindi chote
cha uangalizi tutakuwa huru, hatutafungamana na upande wowote na mwishoni
tutatoa ripoti ambayo itakuwa na mapendekezo ya kusaidia maboresho ya chaguzi
zijazo,” amesema Sargentin ambaye pia ni mbunge kutoka Uholanzi.
“Tutafanya kazi kwa
weledi kwa kufuata viwango na taratibu zinazokubalika kimataifa na Umoja wa
Ulaya. Waangalizi wetu wanazingatia kanuni za maadili kwa wangalizi wa chaguzi
za kimataifa zinazoambatana na tamko la Kimataifa la kanuni za uangalizi wa
uchaguzi la mwaka 2005.”
Amesema kundi la
waangalizi wa muda mrefu 34 walishasambazwa kwenye vituo vya uangalizi tangu
tarehe 27 mwezi huu kuangalia maandalizi yote ya uchaguzi bara na visiwani.
Ameeleza kuwa tayari
kundi la waangalizi hao wa muda mrefu limeanza kukutana na maofisa wa uchaguzi,
wagombea na wawakilishi wa asasi za kiraia na watatuma ripoti ya watakayoyaona
kwa kundi kuu jijini hapa ili watoe tathmini ya kina isiyo na upendeleo.
Moja ya mambo ambayo
waangalizi hao watayaangalia ni uhuru wa vyama vya siasa kufanya mikutano yao
pasipo bugudha na kuvunja sheria, ufanisi wa Tume ya Taifa ya Uchaguzi (NEC),
uhuru wa wananchi kushiriki kwenye mchakato huo na upigaji kura na namna vyombo
vya habari vinavyoripoti vyama na wagombea.