Kipindupindu chatua Singida

Wakazi 11 wa Manispaa ya Singida, wamelazwa kwenye kambi ya Mandewa iliyotengwa kwa ajili ya wagonjwa wa kipindupindu, wakihofiwa kuugua ugonjwa huo.

Tayari watatu kati yao wamethibitika kuwa na kipindupindu.

Akizungumza na waandishi wa habari ofisini kwake jana, Mganga Mkuu wa Manispaa ya Singida, Dk John Mwombeki alisema mgonjwa wa kwanza alipokelewa Septemba 25, mwaka huu na kulazwa katika hospitali ya mkoa.

Alisema mgonjwa huyo alitokea jijini Dar es Salam, Septemba 24.

“Alipolazwa hospitalini na kuchukuliwa vipimo, aligundulika kuwa na kipindupindu na kuanzishiwa matibabu, ambapo kwa sasa anaendelea vizuri huko kwenye kambi,” alisema Dk Mwombeki.

Mganga huyo alisema mgonjwa mwingine alitokea Kijiji cha Ilongero katika Jimbo la Singida Kaskazini na wa tatu alitokea Mtaa wa Majengo Singida mjini.

Dk Mwombeki alisema wagonjwa wengi waliolazwa katika kambi hiyo wanaharisha damu na kutapika.

Pia alitumia fursa hiyo kuwatahadharisha wakazi wa manispaa hiyo kuwa wakiona dalili za ugonjwa huo ikiwamo, kuharisha wafike haraka katika vituo vya afya waweze kupata huduma ya vipimo kujua kama tatizo ni ugonjwa huo.

“Tumeshawatangazia kuwa wahakakikishe wanatumia majisafi na salama, na yachemshwe kwanza kabla ya kutumika. Vyakula hali kadhalaika viliwe vingali vya moto,” alifafanua.

Wakati huohuo, mganga huyo alitoa wito kwa wamiliki wa mabasi, hasa ya masafa marefu wahakikishe wanayafanyia usafi wa kutosha kwenye viti vya abiria ili kuondoa uwezekano wa abiria wengine kuambukizwa kipindupindu.

Alisema kuna uwezekano abiria wenye vimelea vya ugonjwa huo wakaviacha kwenye viti vya mabasi.