Watu 36 wamefariki dunia kwa ugonjwa wa kipindupindu katika
Jiji la Dar es Salaam
tangu Agosti 15.
Manispaa ya Kinondoni inaongoza kwa kuwa na idadi kubwa ya
watu waliokumbwa na kipindupindu kwa kuwa na wagonjwa 1,194; Ilala 996 na
Temeke 71.
Mkurugenzi wa Manispaa ya Kinondoni, Mussa Natty alisema
jana kuwa idadi ya waliokufa kwa kipindupindu katika manispaa hiyo imefikia 17,
huku kukiwa na wagonjwa wapya 15.
Natty alitoa takwimu hizo jana wakati akipokea vifaa na dawa
kwa ajili ya wagonjwa zenye thamani ya Sh15 milioni kutoka Benki ya CRDB baada
ya Mganga Mkuu wa manispaa hiyo, Dk. Aziz Msuya kuomba msaada.
Alisema manispaa hiyo imetumia Sh537 milioni kwa ajili ya
matibabu ya wagonjwa, ikiwamo ununuzi wa vifaa na dawa kwa waliolazwa katika
kambi maalum zilizopo Mburahati.
Awali, Mkurugenzi Mtendaji wa CRDB, Dk Charles Kimei alisema
benki yake imeguswa na idadi ya vifo vinavyotokana na ugonjwa huo.
“Kwa kutambua hali iliyopo Kinondoni, tumeamua kutoa vifaa
tiba na dawa kwa ajili ya wagonjwa waliolazwa,” alisema Dk Kimei na kuongeza:
“Kila mwaka CRDB hutenga asilimia moja ya faida yake kwa ajili ya kusaidia
jamii na kwamba kupitia uzinduzi wa Huduma ya Wiki ya Wateja tumetoa msadaa
huo.”
Mganga Mkuu wa Manispaa ya Ilala, Victorina Ludovick alisema
hadi sasa watu 19 wamefariki dunia tangu ugonjwa huo ulipoingia katika wilaya
hiyo.
“Leo (jana) wagonjwa wapya wapo 28 na waliolazwa katika
kambi ni 43,” alisema.