Mgombea urais kwa tiketi ya Chadema, Edward Lowassa ameeleza
kusikitishwa na kitendo cha polisi kuwapiga mabomu wananchi wa Tanga waliokuwa
wakitoka kwenye mkutano wake.
Lowassa alisema hayo jana kwenye mkutano wa kampeni
uliofanyika Korogwe baada ya juzi kulazimika kuvunja mkutano wake kutokana na
wingi wa watu na kusababisha wananchi wengi kuzimia mjini Tanga.
Baada ya kuvunja mkutano huo, polisi walipiga watu mabomu
ili kuwatawanya jambo ambalo Lowassa alisema limemsikitisha na kuwaomba waache
kufanya hivyo na badala yake watoe ushirikiano kwa wananchi.
“Nasikitika polisi kupiga mabomu. Tushirikiane katika jambo
hili ili kuondoa vurugu,” alisema Lowassa huku akiwashukuru wananchi wa Tanga
kwa mapokezi makubwa aliyoyapata.
Lowassa, ambaye jana alifanya mikutano ya aina yake
akielekea Dar es Salaam kwa gari, alisimamishwa na umati mkubwa wa watu
waliokuwa wametanda barabarani katika Jimbo la Muheza na kuhutubia akiwa juu ya
gari akisema anahitaji kura za kutosha ili aweze kuleta mabadiliko ambayo wananchi
wanayahitaji.
Wananchi hao wa Muheza walimtaka Lowassa awaeleze atafika
lini kufanya mkutano mkubwa hapo na atawasaidiaje kutatua tatizo la kutozwa
ushuru kwa vitu vidogovidogo.
Lowassa aliahidi kulishughulikia tatizo hilo la ushuru kwa kuliwekea utaratibu
maalumu atakapoingia Ikulu na kwamba kabla ya kampeni kuisha, atafika Muheza
kuzungumza na wananchi hao.
Akiwa njiani kwenda Korogwe, Lowassa alikutana na umati
mkubwa wa watu barabarani ambao walikuwa wakielekea Korogwe mjini ambako
alihutubia na kuwaeleza kwa nini ameamua kugombea urais.
Aliwaambia wakazi hao kuwa umaskini umekithiri na mambo kuwa
hovyo, hivyo ameamua kugombea ili kuyashughulikia na atawasaidia katika elimu, afya
na kilimo.
“Hapa mkoani kwenu nitafufua Bandari ya Tanga ambayo ndiyo
itainua uchumi wa mkoa huu,” alisema Lowassa.
Akitokea Korogwe kuelekea Dar es Salaam, umati mkubwa wa
wananchi ulisimamisha msafara wake katika eneo la Michungwani jambo lilimfanya
asimame tena na kuhutubia kwa dakika saba akiwaomba wamchague ili aboreshe
sekta ya elimu na kuifufua Bandari ya Tanga.
Msafara mgombea huyo ulipofika Kabuku ulisimamishwa tena na
polisi walifanya kazi kubwa kuwaweka wananchi pembeni huku magari yakikaa
kwenye foleni na kusubiri Lowassa ahutubie.
Wananchi hao walisema kuwa kuanzia asubuhi walikuwa
wanasubiri ‘mabadiliko’.
Lowassa aliwaomba kura wananchi hao kwa kuwahoji, “mtanipa
kura zenu?” nao wakajibu; “tutakupaaaaaaa”.
Lowassa alisema atawatatulia tatizo la maji ambalo
linawakumba wakazi wa Kabuku kwa muda mrefu.
Wananchi hao walimwonyesha maji wanayokunywa jinsi yalivyo
machafu na baada ya kuyaona alisema wakimpa kura, atahakikisha wanapata
majisafi na salama.
Akiendelea na safari, alikuta umati mwingine wa wananchi
alipofika Komkonga ambako aliwaahidi kushughulikia tatizo la maji na hospitali,
mambo ambayo wananchi wa hapo walimweleza kuwa ni kubwa kwao.
Alitumia dakika tatu kuwaomba kura ili akiwa rais,
awatatulie matatizo yao .
Baadaye alisimama na kuhutubia eneo la Mkata.
Duni na dawa ya
umaskini
Mgombea mwenza wa Chadema, Juma Duni Haji amesema ili
kuondokana na umaskini, kitu kikubwa ni kuwapatia elimu Watanzania na ndiyo
sababu kubwa ya Ukawa kuingiza elimu katika ilani yake.
Akihutubia wananchi katika Mandawa, Kilwa alisema ikiwa
watachaguliwa, Ukawa imepanga suala la elimu kuwa bure. Duni alisema wote
waliopata elimu enzi ya ukoloni, waliondokana na umaskini. “Inasikitisha kuwa
hata baada ya miaka 50 ya uhuru, hali ya Watanzania bado ni maskini.”
Alisema atahakikisha wakulima wa korosho katika mikoa ya
Kusini wanafaidika kutokana na kilimo hicho kwa kusaidiwa kuuza katika masoko
ya kimataifa.