Mgombea urais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kupitia Chama Cha Mapinduzi (CCM), Dk.
John Magufuli, amewataka watumishi wa Bohari ya Dawa (MSD), kukaa mguu sawa kwa
sababu hatakubali kusikia hospitali za serikali zikikosa dawa kama
ilivyo sasa.
Dk. Magufuli alisema inashangaza kuona wananchi wanateseka
kwa kukosa dawa kwenye hospitali za serikali na wagonjwa kuandikiwa kwenda
kununua dawa hizo kwenye mduka binafsi.
Alitoa onyo hilo
jana wilayani Kilindi, mkoani Tanga wakati akiwahutubia wananchi kwenye mkutano
wa kampeni.
“Hawa wanaohusika na
kusambaza madawa wakae mguu sawa maana serikali ya Magufuli haitakubali kuona
wananchi wanaendelea kunyanyasika kwa ukosafu wa dawa wakati kwenye maduka
binafsi zipo,” alisema Dk. Magufuli na kushangiliwa na wananchi hao.
DK. Magufuli alisema hajaomba nafasi ya urais kufanya
majaribio, hivyo watumishi wazembe serikalini wanaokwamisha huduma za maendeleo
ya Watanzania wanapaswa kujitazama upya.
Aidha, Dk. Magufuli alisema Tanzania si maskini kwani ina
raslimali nyingi isipokuwa mafisadi wachache na wengine wakiwa serikalini ndio
wameifikisha nchi pabaya kwa kutumia nafasi zao vibaya.
“Nipeni urais muone
namna nitakavyowashughulikia hawa mafisadi, hawa ndiyo wamesababisha wananchi
wengine kuichukia serikali kwa kuwa wamekuwa wakitumia fedha zao kuwanyanyasa
wananchi wa hali ya chini ambao wanakosa huduma hospitalini,” alisema Dk.
Magufuli.
Mgombea huyo alisema nafasi ya urais inamtosha, hivyo
wasihangaike na wagombea wa vyama vingine ambao alisema wamekuwa wakitoa ahadi
ambazo hawana uwezo wa kuzitekeleza.
“Nafasi ya urais
inanitosha kwa sababu lengo langu ni kuwatumikia Watanzania, najua hapa Songe
mnahitaji lami, nimeweza kujenga kilomita nyingi nchini na madaraja mengi,
siwezi kushindwa kilomita tano za lami
hapa Songe,” alisema.
Katika hatua nyingine, msafara wa Dk. Magufuli uliingia
mkoani Tanga kutoka Morogoro kwa kishindo kutokana na mapokezi makubwa
aliyoyapata kutoka kwa wanachama wa CCM na wananchi wa mkoa huo.
Msafara wa mgombea huyo ambao ulikuwa ukitokea mkoani
Morogoro, ulisimama katika vituo zaidi ya 14 ukiwa njiani kuelekea wilaya ya
Kilindi na Handeni mkoani humo ambapo alikuwa akizungumza na wananchi waliokuwa
wamefurika barabarani wakimsubiri.
Dk. Magufuli alilazimika kusimama njiani na kuzungumza na
wananchi hao na kuwanadi wagombea wa udiwani wa maeneo husika kutoka CCM ambao
walikuwa barabarani na wananchi wakimsubiri kwa muda mrefu.
Mgombea huyo alielezea kufurahishwa na mapokezi hayo ya aina
yake aliyopata mkoani humo na kuahidi kuwa ameondoka na deni na njia pekee ya
kuwalipa wananchi hao ni kuhakikisha anatatua kero zao.