Mgombea urais wa CCM, Dk John Magufuli amewataka Watanzania
wampe kura ili akiingia Ikulu akawafunge mafisadi kwa makufuli.
Dk Magufuli alitoa kauli hiyo jana katika Kijiji cha Mvumi
Mission alipokuwa akihutubia umati wa wananchi waliojitokeza kumsikiliza na
kusisitiza kuwa serikali atakayoiongoza haitakuwa na mchezo wala uonevu kwa
wanyonge.
“Nipeni kura za kutosha ili nikiwa rais, niwafunge mafisadi
kwa makufuli, hapa ni kazi tu,” alisisitiza Dk Magufuli.
Huku akishangiliwa na wananchi waliojitokeza katika Uwanja
wa Mvumi, Dk Magufuli alisema akiingia madarakani atasimamia na kuhakikisha
ujenzi wa barabara kwa kiwango cha lami kutoka Dodoma hadi Mvumi Mission unakamilika.
Aliwatupia vijembe baadhi ya wagombea kutoka vyama vingine
kwamba wamekuwa na tabia ya kubeza maendeleo yaliyofanywa na CCM wakati wanajua
na wanaona.
Awakutanisha Lusinde,
Malecela
Mkutano huo wa Dk Magufuli uliwakutanisha mahasimu wawili
kisiasa, Waziri Mkuu mstaafu, John Malecela na mgombea ubunge wa Mtera,
Livingstone Lusinde ambao kwa muda mrefu wamekuwa hawakai meza moja.
Akizungumza jukwaani, Lusinde alimfananisha Malecela na watu
wenye uvumilivu lakini pia akasema ana afya nzuri kama
ilivyo kwa wastaafu wengine akiwawamo; Joseph Warioba, Dk Salim Ahmed Salim na
hata Rais Jakaya Kikwete ambao alisema bado wanaweza kusimama kwenye majukwaa
kwa muda mrefu.
Lusinde alimshukia Waziri Mkuu mstaafu, Frederick Sumaye
kuwa hana shukurani na kwamba kama ameshindwa
kushiba kipindi akiwa waziri mkuu alichokaa miaka 10, hawezi kushiba kwa sasa.
“Mimi ninaomba Magufuli ukiapishwa tu, tusaidie watu wa
Mtera. Tuna njaa kutokana na mvua ambazo hazikunyesha, tusaidie maji na
mawasiliano katika maeneo yetu, ujenzi wa barabara ya lami Mvumi – Dodoma pamoja na kuiona
kwa karibu wilaya yetu ni kubwa hebu igaweni,” alisema Lusinde.
Malecela ambaye ni makamu mwenyekiti wa CCM mstaafu,
aliwataka Watanzania kuichagua CCM ili iweze kuwapelekea maendeleo.
Aliwauliza wananchi wa Mtera iwapo wangekuwa tayari kuwabeba
Ukawa migongoni, nao wakaitikia kuwa hawako tayari.
Alisema kura za ushindi kwa CCM zinatakiwa kufanyika nyumba
kwa nyumba ili ushindi uwe mkubwa na kuwabeza wapinzani wanaosema chama hicho
hakijafanya kitu wakati kuna barabara za lami kutoka Dar es Salaam hadi Sumbawanga, vitu ambavyo
havikuwapo.
Leo, Dk Magufuli atafanya ziara katika majimbo ya Mpwapwa
Mjini, Kongwa na kuhitimisha katika Uwanja wa Jamhuri mjini Dodoma .
Aahidi barabara
Isimani
Akiwa Iringa, Dk Magufuli aliwaahidi wakazi wa Jimbo la
Isimani kuwa akichaguliwa, atajenga barabara kwa kiwango cha lami kutoka Izazi
– Pawaga - Mlowa mpaka Hifadhi ya Mbuga ya Ruaha.
Pia, alisema atawapatia wafugaji maeneo ya malisho na
kutatua migogoro ya wakulima na wafugaji, uimarishaji miundombinu ya
umwagiliaji na uboreshaji wa Kituo cha afya Tarafa ya Pawaga ili kiwe katika
kiwango cha hospitali.
Dk Magufuli aliwaeleza wananchi kuwa akichaguliwa watarajie
serikali ya awamu ya tano kuwa ya wachapakazi.
Akimnadi mgombea ubunge wa Isimani kupitia CCM, William
Lukuvi alisema, anamfahamu vyema kwa kuwa amekuwa naye katika awamu nyingi
serikalini na ni mchapakazi, hivyo atashirikiana naye kutatua changamoto
zilizopo.
Katika Kijiji cha Migoli alikofanya mkutano wake wa mwisho
mkoani Dodoma ,
Dk Magufuli alikumbushia ahadi ya Sh50 milioni kwa kila kijiji kwa ajili ya
uwezeshaji wa vijana na wanawake.
Alisema ana uzoefu serikalini, hivyo anajua fedha zitatoka
wapi na atahakikisha kila kijiji au kitongoji kinapata mgawo huo.
CCM yalalamikia Ukawa
Katika hatua nyingine, CCM imelalamikia vitendo vya wafuasi
wa Ukawa, kufanya vurugu katika mikutano na misafara ya mgombea wake, Dk
Magufuli kwa kuwa hali hiyo inahatarisha uvunjifu wa amani.
Katika taarifa yake kwa vyombo vya habari, iliyosainiwa na
Mjumbe wa Kamati ya Kampeni, January Makamba jana, CCM ilidai viongozi wa Ukawa
waliwapanga vijana wao maeneo ya Stendi ya Uyole na kumpigia kelele Dk Magufuli
ili asisikike wakati mkoani Tanga walipiga mawe ofisi za mkoa.
“Wafuasi wa CCM wana
uwezo wa kupanga na kufanya hayo, lakini tumekuwa tukihimiza amani na kufanya
hivyo si njia sahihi ya kuomba ridhaa kwa wananchi,” ilisema sehemu ya taarifa
hiyo.
January alisema kuwa
CCM inawasihi Ukawa kufanya kampeni za amani ili kumaliza mchakato kwa amani.
“Tukio la hivi
karibuni la kupigwa mawe ofisi za CCM Tanga na kufanya vurugu, Uyole zimekera,”
alisema.