Nyota watano watemwa Taifa Stars

Kocha msaidizi wa timu ya Taifa ‘Taifa Stars’, Hemmed Morocco ametangaza kikosi cha wachezaji 24 watakaocheza na Malawi huku akiwaengua wachezaji watano waliokuwapo kwenye kikosi kilichoivaa Nigeria mwezi uliopita.

Wachezaji walioenguliwa kwenye kikosi hicho ni Abdi Banda (Simba), Michael Aidan (Ruvu Shooting), Abdurahman Mbambi (Mafunzo), Ramadhan Singano na Ame Ally. 

Akizungumza Dar es Salaam jana, Morocco alisema kikosi hicho kitaingia kambini Oktoba Mosi tayari kujiandaa na mchezo huo wa mtoano wa kuwania kupangwa kwenye makundi ya kugombea tiketi ya kucheza Fainali za Kombe la Dunia 2018 nchini Urusi.

Iwapo Stars itafanikiwa kuitoa Malawi, Tanzania itaingia kwenye raundi ya pili ya kufuzu ambako itamenyana na Algeria. Ikifuzu mtihani wa Algeria, Tanzania itafanikiwa kupangwa kwenye kundi la kuwania tiketi ya kwenda Russia 2018.

Kutokana na kuwa chini kwenye viwango vya Fifa. Tanzania imelazimika kuanza hatua ya awali kwa kumenyana na Malawi, Jumatano ijayo Oktoba 7.

Morocco aliwataja wachezaji ambao wataingia kambini kuivaa Malawi kuwa ni makipa Ally Mustapha ‘Barthez’, Aishi Manula na Said Mohamed wakati walinzi ni Shomari Kapombe, Juma Abdul, Mwinyi Haji, Hassan Isihaka, Mohamed Hussein ‘Tshabalala’, Nadir Haroub ‘Cannavaro’ na Kelvin Yondani.

Kwa upande wa viungo watakaounda kikosi hicho ni Frank Domayo, Salum Telela, Said Ndemla, Deus Kaseke, Mudathir Yahya, na Farid Musa huku washambuliaji wakiwa John Bocco, Rashid Mandawa, Ibrahim Hajib na wachezaji wa kimataifa waliounganishwa kwenye kikosi hicho ni Mbwana Samatta, Thomas Ulimwengu (TP Mazembe- DR Congo) na Mrisho Ngassa (Free State – Afrika Kusini).


Katika hatua nyingine, Morocco amemshauri Mwinyi Kazimoto kuwa umri wake bado ni mdogo kutangaza kuacha kulitumikia taifa na anachokifanya ni kujimaliza.