TUME YA TAIFA YA UCHAGUZI YATAJA TAREHE YA UCHAGUZI LUSHOTO, ULANGA MASHARIKI

TUME ya Taifa ya Uchaguzi inayotarajiwa kusimamia uchaguzi mkuu, Oktoba 25 mwaka huu, imetangaza rasmi siku ya uchaguzi wa majimbo ya Lushoto na Ulanga Mashariki kufuatiwa na vifo vya wagombea wa majimbo hayo.

Akizungumza na wanahabari kwenye ukumbi wa New Africa Hotel jijini Dar es Salaam leo wakati wa mazungumzo na wawakilishi wa watu wenye ulemavu, Mwenyekiti wa Tume ya Taifa ya Uchaguzi, Jaji Damian Lubuva, amesema kuwa tume imepokea taarifa za vifo vya wagombea wa ubunge majimbo ya Lushoto (CHADEMA) na Ulanga Mashariki (CCM).

Amesema kuwa mbali na wagombea hao wa ubunge pia kuna wagombea wanne wa udiwani katika kata za Bomang’ombe-Wilaya ya Hai (CCM), Bukene-Shinyanga (CCM) Msingi-Mkalama Singida (CHADEMA) Muleba (CCM) Uyole –Mbeya (CCM) ambao wamefariki, hivyo chaguzi hizo kuahirishwa hadi tarehe aliyoitaja.

Alisema kwa kufuata sheria na taratibu za tume hiyo, imeona vema mchakato wa uchaguzi kwa majimbo hayo upande wa uteuzi wa wagombea ufanyike Oktoba 12 mwaka huu .

Aidha Lubuva alisema kampeni zitaanza mara baada ya uteuzi wa wagombea wa wabunge na madiwani Oktoba13 hadi Novemba 18 huku uchaguzi ukifanyika Novemba 22 mwaka huu.

Kwa upande wa watu wenye mahitaji maalum kama walemavu alisema kuwa tume tayari imejipanga kuhakikisha kwamba watu walemavu wanapata msaada pindi wawapo kwenye vituo vya kupigia kura, hivyo kwa kuzingatia hilo tume imetoa maelekezo kwa wasimamizi wa vituo na namna ya kuwahudumia mara watakapo fika katika vituo vya kupigia kura ili wapewe kipaumbele.


Vilevile aliongeza kuwa upande wa watu wenye ulemavu wa kutoona tume imeandaa kifaa kijulikanazo kama “Tactile Ballot Folder” kitakachowasaidia kupiga kura pasipo kusaidiwa na mtu yeyote na hivyo kutimiza lengo la usiri wa kura ya mpiga kura.