UTAFITI: Dk Shein anaongoza kwa zaidi ya asilimia 60%

Chama Cha Mapinduzi (CCM) kimesema utafiti kilioufanya tangu kuanza kwa kampeni za Uchaguzi Mkuu wa mwaka huu unaonesha kuwa mgombea urais wa Zanzibar kwa tiketi ya chama hicho, Dk Ali Mohamed Shein anaongoza kwa zaidi ya asilimia 60 dhidi ya wagombea wa vyama vingine.

Akizungumza kwenye ofisi za chama hicho zilizopo Kisiwa Ndui leo, Naibu Katibu Mkuu wa CCM, Vuai Ali Vuai amesema matokeo hayo yametokana na kazi nzuri aliyoifanya Dk Shein katika miaka mitano ya awamu ya kwanza ya uongozi wake.

“Tathmini imeonyesha kuwa mgombea urais wa Zanzibar kupitia CCM anakubalika zaidi kuliko wagombea wote wanaoshiriki kwenye uchaguzi huu na kwa kukisia tayari anaongoza kwa zaidi ya asilimia 60,” amesema Vuai

Ameongeza kuwa tathmini hiyo inaonyesha kuwa Dk Shein anaongoza kutokana na udhaifu wa mgombea wa CUF, Maalim Seif Sharrif Hamad anayegombea kwa mara ya tano bila mafanikio.

Vuai amesema kuwa Dk Shein amewapiku wagombea wengine kutokana na uwezo wake mkubwa wa kusimamia na kutekeleza Ilani ya Uchaguzi ya chama hicho kwa asilimia kubwa.

Tathmini hiyo inaonyesha kuwa CCM inatarajia kupata kura nyingi kutoka Pemba ambako kwa muda mrefu kumekuwa ni ngome ya CUF.


Naibu Katibu Mkuu huyo wa CCM ameeleza kuwa wana CCM katika kisiwa hicho wamekua kidemokrasia hivyo uchaguzi huu hawatatishwa kama ilivyokuwa katika chaguzi zilizotangulia.