Watu watano wamefariki dunia papo hapo kwa kukatwa
katwa mapanga na kuchinjwa kama
wanyama katika kitongoji cha Kisesa kata ya Bugalama wilaya ya Maswa Mkoani
Simiyu.
Watu hao ambao ni wa familia moja walifanyiwa unyama huo kwa
kukatwa katwa mapanga sehemu ya shingoni.
Akizungumza na
waandishi wa habari Kamanda wa polisi Mkoani hapa Gemine Mushy alisema
tukio hilo
lilitokea juzi majira ya saa 9 ambapo Baba, Mama pamoja na watoto wao 3 waliuawa.
Mushy aliwataja waliofanyiwa unyama huo kuwa George Charles
(30) ambaye ni Baba wa familia, Siku John (23) Mama wa Familia na watoto wao
ambao ni Mchambi George (7) Tuma George (5) pamoja na Amos George (Miezi 9)
wote wasukuma wa kitongoji hicho.
Kamanda Mushy alieleza chanzo kuwa ni mgogoro wa ardhi kati
ya marehemu (George) pamoja na Baba yake wa kambo ambaye alinunua kipande cha
ardhi alikokuwa akiishi marehemu.
Aliongeza kuwa baada ya tukio hilo jeshi la polisi lilifanya msako na
kuwakamata watuhumiwa 3 ambao aliwataja kuwa ni Migata Lusalago (50) Jihelya
Migata (30), Solo Kengele (31) wote wasukuma wa kijiji cha Bugalama.
Kamanda mushy alieleza kuwa waliokamatwa ni Baba wa kambo wa
Marehemu pamoja na watoto wake wawili ambao ilidaiwa kuwa wameweza kushiriki
katika kutenda tukio hilo
la kinyama.
Katika hatua nyingine
Mushy alisema kuwa uchunguzi wa
kina unaendelea kufanyika ili kuwapata wahusika zaidi wa tukio hilo .