WHO imetoa muongozo mpya wa matibabu ya UKIMWI

 Shirika la Afya Duniani (WHO) limebadili msimamo wake wa awali ambapo walioathirika na virusi vinavyosababisha ukimwi (HIV) ilibidi wasubiri kuwa wagonjwa kabisa kabla ya kuanza kutumia tembe za kupunguza makali ya ukimwi.

WHO limeagiza kuwa kila mtu anayethibitishwa kuwa ameambukizwa na virusi vinavyosababisha ukimwi, HIV, anapaswa kuanza kupewa matibabu mara moja.

Mwongozo huu mpya unatokana na ushahidi unaoonyesha kuwa watu walio na HIV wanaoanza kutibiwa mara moja huishi kwa muda mrefu zaidi.


 WHO linaamini kuwa mwongozo huu mpya unaweza kupunguza vifo zaidi ya milioni 21 kwa muda wa miongo miwili ijayo.

Ushahidi uliopatikana katika mataifa yanayostawi kama vile Marekani uanonyesha kuwa wagonjwa wengi wanaoanza kutibiwa tu mara wanapogunduliwa kuwa na virusi vya ukimwi huishi muda mrefu zaidi.

Shirika hilo pia linapendekeza kwamba makundi ya watu ambao wako katika hatari kubwa ya kuambukizwa wanapaswa kupewa nafasi ya kwanza kutibiwa hata kabla ya uchunguzi kufanywa.


Muongozo mpya uliotolewa unamaanisha kuwa watu milioni 37 kote duniani ambao wanauguwa UKIMWI wanapaswa kupewa dawa za kupunguza makali ya ukimwi
Kwa sasa, watu milioni 15 tu ndio wanapata dawa hizo kote duniani.

Ushauri wa shirika hilo umeungwa mkono na mashirika ya kutoa misaada ya matibabu.
Hata hivyo shirika hilo limesema kuwa kutibu wagonjwa wengi wapya kutahitaji fedha za ziada.