Wizara ya Dk. Mwakyembe yaongoza kwa urasimu

 Taasisi ya Vyombo vya Habari Kusini mwa Afrika (Misa-Tan) imetoa tuzo kwa Shirika la Nyumba la Taifa (NHC) kwa kuwa taasisi bora ya serikali nchini kwa kutoa taarifa kwa wananchi, huku Wizara ya Ushirikiano wa Afrika Mashariki inayoongozwa na Waziri Dk. Harrison Mwakyembe ikiongoza kwa urasimu wa kutotoa taarifa kwa wananchi.

Mwenyekiti wa Misa-Tan, Simon Berege aliyasema hayo jana jijini Dar es Salaam wakati akitoa ripoti ya utafiti uliofanywa kwa ajili ya kuangalia taasisi za umma namna zinavyotoa taarifa kwa wananchi.
Alisema lengo la utafiti huo ni kuhakikisha uhuru wa habari unatambulika ndani ya Katiba kama haki ya msingi pamoja na kuhamasisha uwazi na uwajibikaji.

Berege alisema lengo jingine la utafiti huo ni kuangalia jinsi gani wananchi wa kawaida wanaweza kupata taarifa muhimu katika taasisi za umma ambazo zinawasaidia kufanya maamuzi sahihi katika maisha yao.

Utafiti huo ambao Juni mwaka huu ulihusisha idara nane za serikali na kati ya hizo mbili zilishiriki mwaka jana.

Alizitaja taasisi za umma zilizofanyiwa utafiti huo kuwa ni Shirika la Nyumba la Taifa (NHC), Ofisi ya Takwimu ya Taifa (NBS), Wizara ya Maliasili na Utalii, Mfuko wa Hifadhi ya Jamii (NSSF), Wizara ya Ardhi na Maendeleo ya Makazi, Wizara ya Ushirikiano wa Afrika Mashariki na Mamlaka ya Mawasiliano Tanzania (TCRA).

Katika utafiti huo, Berege alisema waliwatumia wananchi wa kawaida ambao waliandika barua ama kufika katika taasisi hizo kutaka taarifa mbalimbali na baada ya kufanya hivyo walisubiri kuona ni nani anayejibu kwa haraka.