Wizara ya Maliasili na Utalii imesema hakuna Twiga
aliyetoroshwa kutoka mbuga za wanyama kwenda nje ya nchini na kwamba taarifa na
picha zinazosambaa kwenye mitandao
hazina ukweli wowote.
Kauli hiyo imekuja baada ya picha zinazoonyesha Twiga akiwa
anashushwa kwenye gari tayari kupandishwa kwenye ndege katika mbuga za wanyama
kuenene hivi karibuni kwenye mitandao mbalimbali ya kijamii.
Kati ya picha hizo pia, kuna picha inayoonyesha watu ziadi
ya watano wakiwamo raia wa kigeni wakiwa wamezunguka boksi lililokuwa na Twiga
ndani yake, picha ambazo zimeibua maswali mengi kwa wananchi.
Akitoa ufafanuzi kuhusu picha hizo, Katibu Mkuu Wizara ya
Maliasili na Utalii, Dk Adelhelm Meru amesema picha zinazosambaa kwenye
mitandao zimetengenezwa.
“Nyingine wamepakua
kwenye intaneti kutoka nchi nyingine za Afrika ambazo zinaruhusu kuwinda na
kusafirisha wanyama kama Twiga,”amesema Dk Meru.
“Twiga ni nembo ya
Taifa na hapa kwetu hairuhusiwi kuwinda wala
kusarifisha mnyama huyo, alisema Dk Meru”
Hata hivyo alikiri kuwepo na wageni kutoka nje waliokuja
nchini kwa ajili ya shughuli za uwindaji.
Dk Meru alifafanua kuwa Mfalme kutoka Umoja wa Nchi za
Kiarabu (UAE), alikuwa nchini kwa siku nne, tangu Septemba 24 hadi 29 kwa ajili
ya utalii wa kuwinda.
Amesema mfalme pamoja na watu wengine 137 aliyokuwa
ameongozana nao walitumia ndege tatu. Walipofika katika uwanja wa ndege wa KIA,
waliacha ndege mbili uwanjani hapo na kusafiri na moja kwenda mbugani.
“Walienda kwenye
kitalu walichopewa kibali cha kuwinda huko Luliondo na ndege moja ndiyo maana
watu wameunganisha zile picha ili idhaniwe kuwa waliibeba Twiga,”amesema.