Wizara yakanusha kutoroshwa kwa Twiga

Wizara ya Maliasili na Utalii imesema hakuna Twiga aliyetoroshwa kutoka mbuga za wanyama kwenda nje ya nchini na kwamba taarifa na picha  zinazosambaa kwenye mitandao hazina ukweli wowote.

Kauli hiyo imekuja baada ya picha zinazoonyesha Twiga akiwa anashushwa kwenye gari tayari kupandishwa kwenye ndege katika mbuga za wanyama kuenene hivi karibuni kwenye mitandao mbalimbali ya kijamii.

Kati ya picha hizo pia, kuna picha inayoonyesha watu ziadi ya watano wakiwamo raia wa kigeni wakiwa wamezunguka boksi lililokuwa na Twiga ndani yake, picha ambazo zimeibua maswali mengi kwa wananchi.

Akitoa ufafanuzi kuhusu picha hizo, Katibu Mkuu Wizara ya Maliasili na Utalii, Dk Adelhelm Meru amesema picha zinazosambaa kwenye mitandao zimetengenezwa.

“Nyingine wamepakua kwenye intaneti kutoka nchi nyingine za Afrika ambazo zinaruhusu kuwinda na kusafirisha wanyama kama Twiga,”amesema Dk Meru.

“Twiga ni nembo ya Taifa na hapa kwetu hairuhusiwi kuwinda wala  kusarifisha mnyama huyo, alisema Dk Meru”

Hata hivyo alikiri kuwepo na wageni kutoka nje waliokuja nchini kwa ajili ya shughuli za uwindaji.

Dk Meru alifafanua kuwa Mfalme kutoka Umoja wa Nchi za Kiarabu (UAE), alikuwa nchini kwa siku nne, tangu Septemba 24 hadi 29 kwa ajili ya utalii wa kuwinda.

Amesema mfalme pamoja na watu wengine 137 aliyokuwa ameongozana nao walitumia ndege tatu. Walipofika katika uwanja wa ndege wa KIA, waliacha ndege mbili uwanjani hapo na kusafiri na moja kwenda mbugani.


“Walienda kwenye kitalu walichopewa kibali cha kuwinda huko Luliondo na ndege moja ndiyo maana watu wameunganisha zile picha ili idhaniwe kuwa waliibeba Twiga,”amesema.