F Je, wajua? Baba mdogo zaidi duniani? | Muungwana BLOG

Je, wajua? Baba mdogo zaidi duniani?



     Katika umri wa miaka 13, azaa na binti wa miaka 15
    Wapata mtoto wa kike, baba hajui hata bei ya nepi

 MTOTO mwenye umri wa miaka 13, Alfie Patten, ndiye anayetajwa kuwa baba mdogo zaidi duniani, akiwa amepata mtoto na binti wa umri wa miaka 15, wote wakiwa raia wa Uingereza. Ingawa Alfie ana umri wa miaka 13 lakini ana umbile dogo ambalo kimtazamo anaweza kutafsiriwa kama mtoto wa miaka minane.

Kwa mujibu wa habari iliyochapishwa katika gazeti la The Sun, la nchini Uingereza Februari, mwaka jana, Alfie amepata mtoto na rafiki yake wa kike aitwaye Chantelle Steadman.

Siku moja tu mara baada ya kupata mtoto, Alfie aliulizwa kama anafahamu chochote kuhusu bei ya nepi, naye akajibu; “Nadhani ni gharama kubwa sana, ingawa sijui vizuri mambo haya, sijui kama nitamudu gharama hizo. Wakati mwingine baba yangu hunipa pauni 10 hivi za kutumia (zaidi ya Sh 20,000).”

Alipata mtoto huyo, waliyemwita kwa jina la Maisie, Februari mwaka jana kutokana na kile kilichoelezwa kuwa ni matokeo ya kupinga vitendo vya utoaji mimba miongoni mwa vijana.

Naye Chantelle amenukuliwa akizungumzia namna asivyopenda kuingia katika rekodi ya utoaji mimba akisema; “nilidhani itakuwa vema nikijifungua mtoto.

Alfie anatajwa kuwa na urefu wa futi nne na gazeti la The Sun, lilimnukuu akizungumzia tukio hilo na hasa mwitikio wa familia yake. Anasema: “Pindi mama yangu alipogundua suala hili, nilidhani nitakuwa kwenye mgogoro. Mimi na mwenzangu tulitaka mtoto lakini tulihofia namna mwitikio wa watu utakavyokuwa.

"Sikuwa nafahamu chochote kuhusu maana ya kuwa baba. Nitakuwa mwema, na mwenye kujali."

Tukio hilo lilivuta hisia za wengi na kati ya hao ni wanasiasa nchini Uingereza. Mfano, kiongozi wa chama cha Conservative, David Cameron anazungumzia suala hilo akisema: "Nilipoona picha ya watoto hao wazazi kwenye gazeti, nilianza kuwa na wasiwasi jinsi gani watoto wa enzi hizi hapa Uingereza wameanza kuwa wazazi.

“Natumaini kwamba kwa kiasi fulani watoto hawa watakuwa katika maadili kama wazazi wanaowajibika kifamilia, lakini ukweli ni kwamba kuwa wazazi si suala ambalo walipaswa kuliwaza kwa umri wao."

Naye Waziri Mkuu wa Uingereza, Gordon Brown, alikataa kutoa maoni yake kuhusu tukio hilo lakini akiweka bayana kwamba; “Jambo la muhimu ni hatua zilizochukuliwa na serikali kuhakikisha hakuna mimba za utotoni.”

Baba wa Alfie, Dennis mwenye umri wa miaka 45, naye alizungumzia hali hiyo akisema mwanawe hakuwa katika hali ya uelewa wa kutosha muda mfupi kabla ya mwanawe kuzaliwa na kwamba alipozaliwa, mwanawe huyo alikuwa na shauku kubwa ya kumbeba mtoto mikononi mwake.

Dennis alinukuliwa akisema: “Angeweza kubaki nyumbani akiendelea na michezo yake kama mtoto, lakini alikuwa akijitahidi kufika hospitalini karibu kila siku (baada ya ‘mkewe’ kufikishwa hospitalini kwa ajili ya kujifungua).

Inaelezwa kuwa vijana hao walipeana ujauzito wa mtoto wao, Maisie, baada ya kulala pamoja na kufanya ngono bila kutumia kinga. Waligundua kuwa Chantelle amepata ujauzito baada ya ujauzito huo kufikia umri wa wiki 12, yaani zaidi ya miezi mitatu.

Lakini licha ya kugundua hivyo, alifanya suala hilo la siri hadi ujauzito huo ulipofikisha umri wa wiki sita, baada ya mama wa Chantelle, Penny mwenye miaka 38, kuanza kutilia shaka mwenendo wa binti yake na hasa baada ya kubaini kuwa uzito wake umekuwa ukiongezeka kinyume cha hali ya kawaida.

Alfie, awali aliogopa kuwaeleza hata ndugu zake wa karibu akihofia kuwa ‘stori’ yake ya kuwa baba ikifika shuleni basi anaweza kuwa katika mazingira tata hususan kati yake na rafiki zake wanafunzi.

Chantelle alijifungua salama binti huyo katika Hospitali ya Eastbourne, huko East Sussex, baada ya kulazwa hospitalini hapo kwa saa tano akiwa katika chumba cha kujifungulia, maarufu kama labour. Baada ya kujifungua, binti huyo alilieleza gazeti la The Sun kuwa; “Nimechoka, nilikuwa na wasiwasi sana nikiwa labour lakini sasa nina furaha.”

Akisimulia jinsi yeye na mwanaume wake walivyobaini kuwa ana ujazito, Chantelle alisema ni kutokana na maumivu ya tumbo aliyokuwa akiyahisi na hivyo akiwa na mpenziwe walikwenda kupata ushauri wa daktari

Anasema: "Mimi na Alfie tulikwenda kumwona daktari na baada ya kumweleza akatuuliza kama tumewahi kufanya mapenzi. Mimi nikajibu ndiyo naye akatueleza ni lazima mimi nipimwe ujauzito. Alinipima na kunieleza kuwa mimi ni mjamzito. Nilianza kulia na sikujua cha kufanya. Daktari akanieleza ni lazima nimwambie mama yangu, lakini niliogopa kumwambia.

"Mimi na mwenzangu hatukufikiri kwamba tunahitaji msaada wa wazazi wetu. Unajua ukiwa mjamzito huwezi kufikiria haraka haraka kuwaeleza wazazi wako, kwa sababu akili inayojitokeza ni kwamba wataweza hata kukuua kwa hasira."

Lakini mama yake binti huyo, Penny, alianza kuhisi mwanawe hayuko katika hali ya kawaida mbali na kuongezeka uzito, aligundua kuwa fulana mojawapo kati ya alizokuwa akivaa ilionyesha ‘kitumbo’ chake kujitokeza zaidi ya kawaida.

Kwa upande mwingine, dada wa Alfie, amemlalamikia ndugu yake huyo kutokana na kuwa mzazi katika umri mdogo zaidi, akisema huo ni uzembe wa ovyo.

Dada yake huyo, Nicole mwenye umri wa miaka 19 hata hivyo hakusita kuweka bayana kuwa anaelekeza tuhuma zake kwa baba yao mzazi, kwa kuacha Alfie ampachike ujauzito Chantelle. “Kama si yeye (baba), basi Alfie asingekuwa katika hali hii. Baba yao kwa sasa anaishi na mama wa kambo, Nicola.