SIMBA YAICHAKAZA MAJIMAJI KWA BAO 6-0

Simba imetoa kipigo cha mbwa mwizi leo baada ya kuichapa timu ya Majimaji ya Songea ‘wanalizombe’ kwa goli 6-0 kwenye mchezo wa ligi kuu ya Vodacom Tanzania bara uliochezwa kwenye uwanja wa taifa jijini Dar es Salaam

Vijana wa Msimbazi walianza kupata goli lao mapema kutoka kwa mchezaji wao chipukizi Ibrahim Ajib aliyetupia goli tatu pekeyake (hat-trick)

Kwenye mchezo huo Simkba SC ilianza mchezo kwa kasi kwa kuishambulia mara kwa mara timu ya Majimaji na kupelekea kupata magoli ya mawili ya haraka katika dakika 15 za mwanzo, dakika ya nane na dakika ya 14 yote yakifungwa na Ajib.

Dakika za 15 za katikati ya kipindi cha kwanza mchezo ulitulia na Majimaji wakaonesha uhai kidogo na kufanikiwa kutengeneza nafasi kadhaa lakini safu ya ushambuliaji inayoongozwa na Stamili Mbonde ilishindwa kutumia vyema nafasi hizo kuipa goli Majimaji.

Simba walichachamaa tena dakika ya 15 za mwisho za kipindi cha kwanza na kufanikiwa kupata bao mbili goli la tatu likifungwa na Kiiza kwa shuti kali wakati goli la nne likiwekwa kambani na Ajib kisha timu hizo kwenda mapumziko huku Simba ikiwa mbele kwa goli 4-0 dhidi ya Majimaji.

Kipindi cha pili Simba walifanya mabadiliko kwa kumtoa mfungaji wa hat-trick (Ibrahim) Ajib na nafasi yake kuchukuliwa na Pape Abdoulaye N’daw.

Mabadiliko hayo yaliisaidia Simba kwani dakika ya 79 Simba ilipata bao la tano kupitia kwa Mohamed Hussein Tshabalala kabla ya Hamisi Kiiza kupachika bao la sita dakika ya 81 kipindi cha pili akimalizia kazi nzuri ya Pape N’daw.

Majimaji ilipata goli pekee kupitia kwa Ditram Nchimbi dakika za lalasalama na kuifuta machozi timu yake iliyosafiri kutoka Songea, Ruvuma kuifuata Simba jijini Dar es Salaam.

Simba ndio timu pekee mpaka sasa ambayo imetoa wachezaji waliofunga magoli matatu kwenye kwenye mechi moja (hat-trick) msimu huu ambao ni Hamis Kiiza na Ibrahim Ajib.