Kavumbagu kufuru, Azam yamuuza kwa 200m

Didier Kavumbagu.

RASMI! Hatimaye Azam wamekubali yaishe kwa fowadi wake, Didier Kavumbagu kumuachia kutimkia Ulaya katika moja ya klabu nchini Sweden, lakini wakaweka bayana thamani yake kuwa si chini ya dola 100,000, sawa na Sh milioni 200.

Awali, Kocha wa Azam FC, Muingereza, Stewart Hall, alionekana kukataa kuondoka kwa Kavumbagu lakini sasa amekubali yaishe.

Akizungumza na Championi Jumatatu, Hall alisema juzikati alikutana na viongozi wa ngazi za juu katika kuweka mikakati ya klabu na mojawapo ya mambo hayo ni suala la Kavumbagu kutakiwa Sweden, huku kwa sasa wakimsubiria wakala anayeshughulikia suala lake.

Alifafanua kuwa, mbali na maamuzi yao kama klabu, pia Waswidishi hao watabanwa na mkataba wa staa huyo wa zamani wa Yanga wenye kipengele cha thamani yake kutoshuka zaidi ya dola laki moja.

“Ishu ya Kavumbagu ni kwamba tumeamua kumuachia, kwa sasa kinachosubiriwa ni mawasiliano ya wakala anayelishughulikia suala lake lakini msimamo wangu kama kocha na uongozi wa timu kwa ujumla ni kwamba thamani yake haiwezi kushuka chini ya dola laki moja.

“Hata mkataba wake ndivyo unavyosema kuwa iwapo atataka kuuzwa thamani yake ndiyo hiyo. Kama watakuwa tayari, ataondoka, vinginevyo atarudi katika mipango yangu ya baadaye kwa ajili ya michuano iliyopo mbele yetu,” alisema Muingereza huyo.

Hall aligeuka mbogo alipolizwa kuhusiana na nyota wake tegemeo, Pascal Wawa na Kipre Tchetche kutakiwa Jangwani, ambapo alisema hakuna kitu kama hicho.

Mbali na Kavumbagu anayeuzwa, kinda Farid Mussa kwa mujibu wa Hall huenda akatimkia Denmark kwa majaribio huku Mudathir Yahya akiwa 50-50% naye kwenda huko kwa majaribio.