Mawaziri Cuf sasa wadaiwa kulipwa mishahara bila kufanyakazi Zanzibar

Wizara ya Fedha Zanzibar imesema mawaziri wa Chama cha Wananchi (Cuf) wanaounda Serikali ya Umoja wa Kitaifa (Suk), wanaendelea kupokea mishahara na marupurupu kama kawaida licha ya kujivua nyadhifa zao kwa madai utawala wa Rais Dk. Ali Mohamed Shein umefika kikomo Novemba 2, mwaka huu.

Hayo yalisemwa na Naibu Katibu Mkuu wa wizara hiyo, Juma Ameir Hafidh, wakati akizungumza na Nipashe, visiwani humo mwishoni mwa wiki.

Alisema mawaziri hao wa Cuf na manaibu wao wamepokea mishahara na marupurupu ya mwezi Oktoba, mwaka huu licha ya kutangaza kujivua nyadhifa zao.

Alisema kwa mujibu wa kifungu cha 28 (1) (a) cha Katiba ya Zanzibar ya Mwaka 1984, Rais Dk. Ali Mohamed Shein bado ni kiongozi halali hadi hapo Rais mpya atapochaguliwa na kuapishwa kushika wadhifa huo.

“Kimsingi mawaziri wanane na manaibu waziri watatu kutoka Cuf mpaka sasa hakuna aliyeandika barua ya kuachia wadhifa wake pamoja na kukabidhi mali za serikali kwa utaratibu wa makabidhiano.

Kumbukumbu zinaonyesha ni waziri mmoja tu kutoka Cuf ndiye aliyeandika barua ya kujiuzulu wadhifa wake, Juma Duni Haji, wakati  akiwa Waziri wa Miundombinu na Mawasiliano baada ya kuchaguliwa kuwa Mgombea Mweza wa Urais wa Ukawa kupitia Chadema uchaguzi mkuu wa mwaka huu.

“Hakuna waziri mwengine wa Cuf aliyejiuzulu, wote wanalipwa stahiki zao kama kawaida na wala hakuna aliyerudisha fedha za mshahara au marupurupu,” alisema.

Hafidh alisema mawaziri wote wa Suk na manaibu wao wataendelea kulipwa na serikali stahiki zao hadi hapo Rais mpya atakapochaguliwa na kuapishwa kwani muda wao utakuwa umemalizika rasmi na kusubiri baraza jipya la mawaziri kuundwa.

Hata hivyo, Waziri wa Nchi Ofisi ya Makamu wa Kwanza wa Rais wa Zanzibar kupitia Cuf, Fatma Abdulhabib Fereji, alisema kwa mujibu wa kifungu cha 28 (2) (a), wao siyo mawaziri tena kutokana na serikali ya awamu ya saba kufikisha kikomo chake cha miaka mitano ya kubakia madarakani.

 “Sie siyo mawaziri tena na tangu tujivue nyadhifa zetu hatujapokea mishahara wa posho siyo kweli kuwa tumepokea,” alisema Fereji na kuongeza:

“Mie tangu Oktoba 25, mwaka huu nimerejesha vifaa vyote ikiwamo gari na wala siendi tena ofisini kwani Rais muda wake wa kukaa madarakani umekwisha na mimi muda wa kuwa waziri umemalizika tangu Novemba 2, mwaka huu.”