Upotevu wa Makontena 349 Bandarini: Watu 12 Watiwa Mbaroni na Jeshi la Polisi

Kufuatia agizo la Waziri Mkuu Mhe. Kassim Majaliwa la kuwataka watuhumiwa wa wizi wa makontena 329 katika bandari ya Dar es salaam kuchukuliwa hatua na Jeshi la Polisi, tayari Jeshi hilo limewashikilia watuhumiwa kumi na mbili wanaohusika na wizi huo.

Akiongea na waandishi wa habari leo Jijini Dar es salaam,  Mkurugenzi wa Upelelezi wa Makosa ya Jinai (CP) Diwani Athumani amesema kuwa, uchunguzi unaofanywa na wataalamu waliobobea katika makosa ya uhalifu wa kifedha umeweza kuwabaini watu kumi na mbili  ambao wamehusika na wizi huo.

“Kati ya watuhumiwa hao kumi na mbili, watano wanashikiliwa na Jeshi la Polisi na saba bado wapo katika upepelezi na upelelezi utakapokamilika watafikishwa mahakamani,” alisema Kamanda Athumani.

Wanaoshikiliwa kutokana na tuhuma mbalimbali ni Kamishna wa Idara ya Forodha na Ushuru TRA Bw. Tiagi Masamaki, Meneja Kitengo cha Huduma za Ushuru  na Bi.  Habib Mponezia, Msimamizi Mkuu wa Kitengo cha Ushuru wa Forodha.

Watuhumiwa wengine ni pamoja na Bi. Eliaichi Mrema, Msimamizi Kitengo cha Mawasiliano ya Kompyuta  Bw. Haroun  Mpande na Mchambuzi Mwandamizi wa Masuala ya Biashara Bw. Hamis Omary.

Aidha Kamanda Athumani amewaomba wananchi wenye taarifa za ubadhilifu wa mali za Umma kuendelea kulisaidia Jeshi la Polisi katika kutekeleza majukumu yake.