Karibu Mwaka Mpya 2016, Mwaka wa Matumaini Mapya Kwa Watanzania

Mwaka 2016 ni mwaka wa matumaini mapya kwa Watanzania wote walioanza kukata tamaa ya maisha bora. Biashara nyingi zimefilisika kutokana na vikwazo mbalimbali.

Familia nyingi zimeparaganyika kutokana na kukithiri kwa mmomonyoko wa maadili ya kitaifa na kunyauka kwa utu wa ubinadamu uliochochewa na hali duni ya maisha miongoni mwa jamii.

Watu masikini na wenye kipato cha chini wameendelea kukosa mtetezi.

Mwaka 2015, wazee wenye umri zaidi ya miaka 65, ambao hawazidi milioni mbili na nusu hapa nchini, kwa muda mrefu walipaza kilio chao kuhusu haki yao ya msingi ya kupata ‘mrejesho wa hifadhi ya jamii baada ya kulitumikia Taifa lao kwa zaidi ya miongo sita, lakini hakuna aliyewasikiliza.

Huduma za afya ya msingi zilizidi kuwa duni zaidi katika hospitali na vituo mbalimbali vya afya nchini. Kiwango duni cha elimu na mitalaa iliyopoteza mwelekeo, ni baadhi ya vizingiti vilivyoikwaza sekta ya elimu.

Ile dhana ya kikoloni ya kuwalipa wafanyakazi ujira mdogo au mishahara kiduchu au ya kiwango cha chini isiyozingatia utu wa binadamu, iliendelea kukumbatiwa na awamu zilizotangulia.

Kutokana na haya yote, siyo jambo la ajabu , kuikuta Tanzania ikishika nafasi ya 151 miongoni mwa nchi 170 duniani, kwa kiwango cha chini cha hali ya ubora wa maisha ya watu wake.

Shirika la Maendeleo la Umoja wa Mataifa (UNDP) , katika Ripoti yake ya mwaka 2015 , iliyotoa matokeo ya tathmini za utafiti uliofanyika katika nchi wanachama, ilidhihirisha wazi jinsi ambavyo hata nchi zenye kipato kikubwa zilivyoshindwa kutumia utajiri wake ili kuboresha hali ya maisha ya watu wake.

Utafiti huo uliangazia katika maeneo makuu matatu; huduma za afya, ubora wa elimu na viwango vya mapato.

Nchi nyingi zilizojikuta katika kundi la nchi zenye kiwango cha chini cha ubora wa hali ya maisha ya watu wake, zilitoka bara la Afrika, baadhi yake zikiwa na utajiri mkubwa wa maliasili na rasilimali.

Katika kundi hilo, Kenya ilionekana kuwa na unafuu zaidi kwa kupata kiwango cha 0.548 (HDI) na kuongoza kundi hilo lenye nchi 44.

Nchi iliyoshika mkia katika kundi hilo ni Niger, iliyopata kiwango cha 0.348 , ikilinganishwa na viwango vya juu vilivyoshikwa na nchi ya Norway (HDI 0.944) na Mauritius iliyoongoza katika nchi za bara la Afrika kwa kiwango cha HDI 0.777.

Ripoti hiyo inabainisha pia kwamba katika miaka 25 iliyopita, karibu watu wapatao bilioni mbili kutoka nchi mbalimbali, walifanikiwa kujinasua kutoka katika kundi la nchi zenye kiwango cha chini cha ubora wa hali ya maisha.

Tanzania yenye watu wapatao milioni 45, kuendelea kubaki katika kundi la nchi 44 zenye kiwango cha chini cha ubora wa hali ya maisha ya watu wake, ni kiashiria cha wazi cha kushindwa kwa sera, mifumo na mikakati yake ya matumizi sahihi na makini ya maliasili na rasilimali zake

Kwa mtazamo mwingine ni kwamba, Tanzania ilishindwa kuwa sehemu ya nchi hizo zenye watu bilioni mbili waliofanikiwa kujinasua kutoka katika kundi hilo la ubora wa chini.

Mwaka 2016
Kwa nini mwaka 2016 unaweza kuwa Tumaini Jipya na  mwanzo mzuri wa safari ndefu ya kiuchumi kwa Tanzania?

Matumaini yote ya Watanzania yapo mikononi mwa uongozi wa Serikali ya awamu ya tano.

Kila Mtanzania anatarajia labda uongozi huu utakuja na kitu kipya katika maisha yao, ambacho kilisahaulika kwa miaka mingi. Nacho ni kutokomeza ufukara na umasikini wa kipato kwa vitendo.

Kama miaka 25 iliyopita tumeipoteza bila ya kufikia malengo tuliojiwekea, kutokana na sababu mbalimbali, hatuna sababu tena ya kupoteza miaka mingine 25 ijayo.

Hata hivyo, uongozi mpya wa awamu ya tano, umeanza kuonyesha dalili njema za kukabiliana na adha hiyo.

Serikali ya sasa imerithi uchumi ukiwa katika hali duni na tegemezi, huku taasisi nyingi za umma au za Serikali zikiwa hazifanyi vizuri kama ilivyo kusudiwa. Rushwa na ufisadi navyo vimetapakaa katika kila nyanja ya maisha yetu.

Yote hayo yanafanyika Tanzania ikiwa miongoni mwa nchi chache barani Afrika zilizobahatika kuwa na utajiri mkubwa wa maliasili na rasilimali mbalimbali.

Mtu yeyote aliye na dhamira ya kufunga safari, tena safari ndefu, kwanza lazima ajue wapi anakotaka kwenda. Akisha jua wapi anakotaka kwenda, pili, lazima ajue njia atakayopita na namna ya kumfikisha huko alikokusudia kwenda.

Uongozi mpya wa awamu ya tano, utalazimika kuangalia nyuma tulikotoka (miaka 25 iliyopita). Kisha utafakari, tunaitaka Tanzania ya aina gani miaka 25 ijayo?